01/05/2021
AINA ZA UNAFIKI
Unafiki uko wa aina mbili:
(1)Unafiki wa kiitikadi. (2)Unafiki wa kimatendo.
1. Unafiki wa kiitikadi
Huu unapatikana kwa kuficha Ushirikina na Kudhihirisha Uislamu, na huu ndio uliotajwa katika Qur-ani.
2. Unafiki wa kimatendo
Huu unapatikana kwa kuyaendea kinyume maneno kwa vitendo, basi mwenye kufanya Kosa kubwa kwa kuacha lilioamrishwa au kufanya lililokatazwa atakua ni Mnafiki, mwenye kuacha Sala kwa uvivu, na Zaka kwa ubakhili, na mwenye kufanya Uzinifu, na mwenye kula Riba na mfano wa hayo, wote hao ni wanafiki.
Na kwa Ujumla Mtu akifikia ukubwa na anazo akili (Mukallafu) ima atakua ni Muumini au atakua ni Kafiri, na wala hakuna nafasi baina ya haya mawili.
﴿إِنَّا هَدَيْنَـٰهُ ٱلسَّبِيلَ إِمَّا شَاكِراً وَإِمَّا كَفُوراً﴾
﴾Hakika sisi tumemuongoza Njia ima atakua ni mwenye kushuru na ima atakua ni mwenye kukufuru﴿
[Insaan 3]
Basi Ukafiri kwa mujibu wa lugha ni kuficha na kuziba, nao kwa mujibu wa Sheria umegawika aina mbili Ukafiri wa Kishirikina, -((na Ushirikina uko aina mbili wa kukataa na kufanya usawa))-, na Ukafiri wa Neema.
Basi mwenye kufanya Kosa kubwa ambalo sio Ushirikina atakua ni Kafiri wa Ukafiri wa Neema, ni Mpotevu wa Njia anafanya lisilokua zuri.
Na Unafiki unatembea baina ya Kufuru mbili, basi huo ni Ukafiri wa Ushirikina kwa kuuficha kwake Ushirikina, na huo ni Ukafiri wa Neema kwa kuyaendea kinyume Matendo.
Na Hukumu za Wanafiki katika maisha yetu ya Kidunia ni Hukumu za Waislamu katika Kuoana na Kurithiana na Kuhifadhika Nafsi na Mali, na Allah anajua zaidi.