07/09/2025
Swali: Je, padre sakramenti saba za Kanisa Katoliki ziliasisiwa kweli na Yesu Kristo au ni utunzi na ubunifu wa Kanisa Katoliki tu? Je, unaweza kuonesha nukuu zozote za Biblia?
Jibu na mzee wenu Pd. Titus Amigu.
Sakramenti saba za Kanisa Katoliki ziliasisiwa kweli na Yesu Kristo na hivyo siyo utunzi na ubunifu wa Kanisa Katoliki. Sasa naonesha nukuu za Biblia zinazohusika k**a ifuatavyo:
1. Ubatizo
Sakramenti ya ubatizo iliasisiwa na Yesu pale alipobatizwa mwenyewe mtoni Yordani hivyo akayabariki maji kwa ubatizo wa wanadamu (Mt 3:13-17, Mk 1:9-11, Lk 3:21-22) na baadaye akaamuru mitume wakabatize watu (Mt 28:18-20).
Kuhusu kiasi cha maji, wafuasi walishaelewa kwamba hata maji kidogo yalitosha ndiyo maana watu 3000 siku ya Pentekoste walibatizwa kwa maji machache (Mdo 2:41-42). Si wao tu, Mtume Paulo alibatizwa kwa maji kidogo (Mdo 9:17-19) na bwana jela na familia yake walibatizwa pia kwa maji kidogo (Mdo 16:33). Maji mengi yakiwapo yanaweza kutumika (Mdo 8:34-39) lakini si lazima kwa sababu ubatizo si maji wala suala la kuoshana uchafu wa nje isipokuwa ni nia ya rohoni kumfuasa Mungu (1 Pet 3:21). Tupeane onyo la kiroho: mtu asibatizwe kwa maji mengi siku hizi na kukufuru kwa kutaka kusema ubatizo wake ni bora kuliko ubatizo wa Wakristo 3000 wa siku ya Pentekoste au bora zaidi ya ubatizo wa Mtume Paulo na wa bwana jela na familia yake.
2. Kipaimara
Sakramenti hii iliasisiwa pale mitume walipopewa Roho Mtakatifu ambaye waliweza kuwapokeza wengine kwa kuwawekea mikono, rejea Yn 20:22 na Mdo 8:14-24). Waliadhimisha sakramenti hii kwa namna bayana kabisa kwa watu wa Samaria k**a tunavyosoma katika Mdo 8:14-24.
3. Ekaristi Takatifu
Sakramenti hii ilidokezwa kwa mbali katika chakula cha ajabu kilichoitwa manna walichopewa Waisraeli kwa miaka arobaini jangwani (K*t 16:1-36); iliashiriwa kwa karibu katika miujiza ya kuwalisha watu wengi mikate (Mt 14:13-21, Mk 6:30-44, Lk 9:10-17, Yn 6:1-15); ILIASISIWA KATIKA KARAMU YA MWISHO (Mk 14:12-26, 1Kor 11:23-32) na iliamriwa itumike na Wakristo wote. Yesu alisema watakaokula mwili wake na kunywa damu yake watakuwa na uzima wa milele naye atawafufua siku ya mwisho (Yn 6:35.47-69). Yesu hawatanii wanadamu, hivyo maneno yaliyo katika Yn 6 hakutania bali alimaanisha hivyo hivyo alivyosema.
Watu wasio na sakramenti ya Ekaristi Takatifu na wasiokula mwili wa Yesu na kunywa damu yake wanayaweka maisha yao wenyewe rehani. K**a wanajua alichosema Yesu na wanapuuza ni wakaidi; k**a hawajui alichosema Yesu ni wajinga, ila wana ujinga unaoshindika. Lakini basi hata wasio na Ekaristi Takatifu na wasioipokea wataweza kuupata uzima wa milele kwa sababu ya uwingi na ukuu wa rehema ya Mungu tu kwa vile atawapima kwa huruma kwa kigezo cha pekee, ndicho kigezo cha kusikiliza dhamiri zao tu (Rum 2:12-15). Kisingelikuwapo kigezo hiki, watu hao wasingekuwa na chao tena.
4. Kitubio
Mintarafu sakramenti hii tunaeleza ifuatavyo. Nguvu ya kuondoa dhambi ni ya Mungu (Mk 2:1-12) lakini kwa hiyari yake aliwapasia wanadamu nguvu (ufunguo) hiyo waitumie kwa niaba yake na hivyo kuasisi sakramenti ya Kitubio (Yn 20:19-23). Kwa kuwa ufunguo amewapatia wanadamu, wanadamu hawana budi kwenda kuungama kwa hao waliokabidhiwa ufunguo (Isa 1:18-20). Kuwakimbia au kugoma kuwatumia waliokabidhiwa ufunguo ni ukaidi.
5. Mpako wa Wagonjwa
Yesu aliasisi sakramenti hii pale alipowaamuru mitume na wafuasi wake wakawawekee mikono wagonjwa na kuwapaka mafuta (Mt 10:8, Mk 6:7-13, Lk 9:2). Baada ya kupaa Yesu mbinguni, mitume waliendelea kuiadhimisha sakramenti hiyo kwa wagonjwa kwa ufahamu kamili (Yak 5:13-18).
6. Ndoa
Yesu aliiasisi sakramenti ya ndoa pale alipohudhuria harusi ya Kana na kwa uwapo wake kuikubali taasisi ya ndoa na kuleta baraka juu yake (Yn 2:1-12).
7. Upadre
Yesu aliiasisi sakramenti ya Upadre au Daraja pale alipoamuru mitume wawe wanarudia adhimisho la Ekaristi Takatifu, yaani kwa kule kusema βFANYENI HIVI KWA UKUMBUSHO WANGUβ k**a anavyotueleza vizuri mtume Paulo kwamba ndivyo ilivyopokezwa na wale waliokuwapo sakramenti hiyo inaasisiwa (1Kor 11:23-25). Huwezi kuwaamuru watu warudie kitu kwa kudumu k**a watu hao si wa kudumu. Hapa rejea muktadha wa karamu ya mwisho yenyewe (Mt 26:26-28, Mk 14:22-24, 1Kor 11:23-25).
Hatima
Hadi hapa natumaini jibu limekaa vizuri na limekutosheleza msomaji wangu. Watu wanaodhani kwamba sakramenti zilibuniwa na Kanisa Katoliki wanasigina aya hizo zote na wanasoma Biblia kwa raghba wakimfuata Padre Martin Luther aliyekuwa akisoma Biblia kwa makengeza ilmradi asimame kinyume na mafundisho ya Kanisa Katoliki. Ulikuwa mkasa mbaya wa kati ya mwaka 1517-1520. Ushahidi wa jazba yake ni kukosa kuziona na kushonanisha aya hizo za Biblia zilizokuwa wazi kabisa katika Biblia iliyokuwa mkononi mwake. Unapata picha? K**a si jazba ya ubishi, hivi Martin Luther alishindwaje kuziona aya hizo huku akijinasibu kuisoma sana Biblia? Lakini ukiona mtu halioni gari kubwa lililosimama mbele yake ila anakwambia anaweza kuiona sindano iliyolala mchangani ujue umekumbana na kiroja. Lakini mbaya zaidi ni pale wafuasi wa mtu aliyezifunika aya za wazi za Biblia wanapodai kwamba na wao pia hawazioni. Alahaula! Akili ya kuambiwa ilipasa kuongezewa na yako mwenyewe!