01/01/2019
MKESHA WA MWAKA MPYA; KMT Dayosisi ya Mashariki, Sinza, Dar es Salaam:
Usiku wa jana tumekesha kwa nyimbo za kusifu na kuabudu tukiongozwa na kwaya za KMT Upanga, Sinza, Tegeta, Nyantira na Praise Team.
Askofu Nelson Kisare Mwenyekiti wa Dayosisi ya Mashariki akitoa NENO la ufunguzi aliwaasa Kanisa la Mennonite kuwapa vijana uhuru wa kumwabudu Mungu bila kuigeuza Biblia na maagizo ya Maandiko Matakatifu, maana dunia inabadilika lakini Biblia haibadiliki. Aliwaasa vijana kuepuka kuibeba dunia na mambo yake na kuyaleta Kanisani bali walibebe Kanisa na kulipeleka duniani. Imani ya Kikristo igeuze utamaduni, mila na desturi za dunia na si kinyume chake.
Mchungaji Juma Aguttu (Katibu wa Afya Hospitali ya Shirati) alinena ujumbe wa mkesha kupitia Yoshua 4:1-8 uliobeba MAWE 12 ambayo ni Kanuni 12 za kutembelea mwaka 2019 ili kufikia malengo ya kila mmoja na Kanisa na hata Taifa. 1. Mungu ni Mwanzo wa kila kitu. 2.Kutenda HAKI 3. Kuutegemea Ufalme uliokamilika wa UTATU MT. 4. Beba Silaha za vita 5. Ng'ang'ania usikate tamaa 6. Tambua roho ya uharibifu uikabili 7. Ufalme utatekwa na wenye BIDII 8. Mwanzo mpya 2019. 9. Shukuruni kwa kila jambo 10. Baraka hutoka kwa BWANA 11. Beba MAONO yako 12. Kulea watoto wairithi kazi ya Bwana.
Kanisa lilitoa sadaka ya kwanza (MALIMBUKO) ya mwaka 2019 kisha Kanisa tuliomba maombi ya Shukrani ya 2018, Kuweka wakfu mwaka 2019, Kuombea Umoja wa Kanisa, Uamusho na Kumpokea Roho Mtakatifu, pamoja na maombi ya Kuutafuta Ufalme wa Mungu ili tufunguliwe mipenyo ya mafanikio 2019.
Mchungaji Magasi Mkuu wa Jimbo la KMT Sinza, aliwashukuru wote waliojitoa kuuandaa mkesha huu wa aina yake uliokutanisha waumini wengi wa Dar es Salaam.
Katibu Mkuu KMT Baraza, Mch John Wambura katika kufunga Mkesha huu aliwakumbusha Vijana wa KMT kuwarudisha vijana wenzao waliohamia makanisa mengine na huduma za watu binafsi kuwa warudi maana huku kwetu nako kumenoga sasa. Alikumbusha Kanisa juu ya Dira yetu "Vision 2034" na kuwataka Vijana kuweka alama kwa kushiriki utekelezaji wake. Aliwahimiza vijana wa Mashariki kumsaidia Askofu kwenda Ruvuma mkoa wa Kuenea unaoratibiwa na dayosisi hii. Aliwakumbusha Kanisa kuwa Mwezi May 2019 tutaadhimisha WEEK YA KMT mkoani dodoma Dayosisi ya Kati, hivyo aliwataka waumini kujiandaa kushiriki. Pamoja na hayo alikumbusha Kanisa kuwa Mwaka 2021 kutakuwa na Mkutano wa Wamennonite Duniani (MWC) utakaofanyika Indonesia. Aliwaomba kanisa kujipanga kushiriki na hasa msisitizo ni kwa uwakilishi wa Team ya Praise & Worship ya KMT ipate kushiriki.
Mwisho Askofu Kisare Alitangaza kuwa kuanzia sasa Mkesha huu utakuwa ni sehemu ya matukio katika kalenda ya Dayosisi ya Mashariki na utazunguka majimbo yote. HONGERA KMT SINZA IMEWEZEKANA KWA MARA YA PILI KUWA NA MKESHA MKUBWA WENYE MGUSO WA AINA YAKE.