01/06/2026
Wahitaji 160 Wanufaika na Huduma za Diakonia Himo
MOSHI
Katika juhudi za kuwasaidia wenye uhitaji, jumla ya watu 160, wakiwemo wazee, watoto, na watu wenye ulemavu, wamepatiwa misaada mbalimbali ikiwemo matibabu bure pamoja na mahitaji mengine ya nyumbani , huku watoto zaidi ya 100 wakigharamiwa ada na michango mingine ya shule.
Msaada huo umetolewa wakati wa Ibada Maalumu ya Diakonia iliyofanyika kwa mara ya tano sasa katika Usharika wa Himo, Jimbo la Kilimanjaro Mashariki, Dayosisi ya Kaskazini ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT).
Akizungumza katika ibada hiyo mchungaji kiongozi wa usharika huo George Mamuya amesema , jumla ya wahitaji 160 wamepatiwa huduma za afya ikiwemo matibabu na dawa, huku watoto wakilipiwa ada pamoja na michango ya shule ili kuwawezesha kuendelea na masomo.
Mwenyekiti wa Diakonia katika Usharika huo wa Himo, Dorkasi Moshi, ameeleza kuwa changamoto kubwa wanayokabiliana nayo kwa sasa ni ongezeko la kasi la watu wenye shida ambapo amesema maadhimisho ya Siku ya Diakonia husaidia kwa kiasi kikubwa kukusanya nguvu ya pamoja ili kuwafikia wahitaji wengi zaidi.
Baadhi ya wazee pamoja watu wenye mahitaji maalumu wameeleza kufurahishwa na huduma hiyo wakitaja kuwa faraja kubwa kwao, kwani licha ya misaada ya vitu walivyopewa, fursa ya kukusanyika, kusali pamoja, na kujisikia sehemu ya jamii imewapa nguvu mpya na kuwatoa katika upweke unaowakabili.