UMOJA DAIMA MEDIA

UMOJA DAIMA MEDIA UMOJA DAIMA MEDIA
Official account
We are Christian media organization owned by ELCT NORTHERN DIOCESE

31/05/2026

HARAMBEE YA UJENZI WA NYUMBA YA IBADA KILIMA MOJA, MILIONI 127 ZAPATIKANA

Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Askofu Dkt. Fredrick Onael Shoo, leo Mei 31, 2026 ameongoza harambee ya ujenzi wa Nyumba ya Ibada katika Usharika wa Kilima Moja Mtaa wa Kibaoni-Ebenezer, Jimbo la Karatu.

Katika ibada hiyo, Askofu Shoo alimshukuru Mungu kwa kuwakutanisha waumini kuabudu pamoja na kuwapongeza viongozi na washirika kwa hatua nzuri iliyofikiwa ya ujenzi

Akihubiri katika Siku ya Utatu Mtakatifu, Askofu Shoo alimtaja Nehemia k**a mfano wa ujasiri na imani katika kutekeleza kazi ya Mungu licha ya vikwazo. Alisisitiza kuwa ujenzi wa Nyumba ya Mungu ni jukumu la waumini wote na kwamba kila mmoja anapaswa kuchangia kwa uwezo wake, kwa hiari na kwa furaha.

Aliwahimiza waumini kutokata tamaa wala kusikiliza maneno ya kukatisha tamaa, akieleza kuwa kazi inayosindikizwa na maombi haiwezi kushindwa. Pia alisisitiza umuhimu wa umoja, akisema kuwa umoja ndiyo siri ya mafanikio katika kazi ya Mungu.

Askofu Shoo aliwataka waumini kuendelea kushiriki kwa fedha, nguvu kazi na maombi ili kuhakikisha ujenzi huo unakamilika kwa utukufu wa Mungu. Alimalizia kwa kuwakumbusha kuwa kwa Mungu hakuna lisilowezekana.

Mchungaji Kiongozi wa Usharika huo, Goodluck Kwayu, katika risala yake, amesema kuwa ziara ya leo ya Askofu Shoo ni ya kihistoria, akiifananisha na huduma aliyopewa Nehemia ya kusimamia ujenzi wa nyumba ya Mungu.

Amesema Askofu Shoo ameona uhitaji uliopo katika Usharika wa Kilimamoja na kwamba umoja na ushirikiano vitasaidia kutimiza agizo la Yesu Kristo la kufanya mataifa yote kuwa wanafunzi wake.

Mchungaji Kwayu ameeleza kuwa ujenzi wa hekalu umefikia hatua ya sasa kutokana na mchango wa waumini wachache pamoja na marafiki wa usharika. Amesema hatua inayofuata ni upauzi wa jengo, ambao unatarajiwa kugharimu shilingi milioni 62.

Aidha, amesema harambee ya leo inalenga kukusanya jumla ya shilingi milioni 192 kwa ajili ya kukamilisha miradi mbalimbali ya maendeleo katika Usharika wa Kilimamoja. Kipaumbele kikubwa ni kukusanya zaidi ya shilingi milioni 62 kwa ajili ya upauzi wa jengo la mtaa wa Kibaoni–Ebenezer, ambao ndio mtaa pekee ambao jengo lake bado halijapauliwa.

21/05/2026

KKKT Dayosisi ya Kaskazini na Magharibi Kati Wasaini Makubaliano ya Ushirikiano

KKKT Dayosisi ya Kaskazini na KKKT Dayosisi ya Magharibi Kati leo Mei 21, 2026 zimesaini rasmi makubaliano ya ushirikiano katika hafla iliyofanyika katika Ofisi Kuu za Dayosisi ya Kaskazini.
Makubaliano hayo yalisainiwa na Mkuu wa Dayosisi ya Kaskazini, Askofu Dkt. Fredrick Onael Shoo pamoja na Katibu Mkuu Mhandisi Zebadiah Moshi kwa upande wa Dayosisi ya Kaskazini.

Kwa upande wa KKKT Dayosisi ya Magharibi Kati, makubaliano hayo yalisainiwa na Askofu Dkt. Isack Kisiri Laizer pamoja na Katibu Mkuu Mch. Baraka Mungure.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini Mhandisi Moshi, amesema ushirikiano huo unalenga kukuza malezi ya maisha, kuimarisha imani, umoja na huduma za kanisa.

Aidha, makubaliano hayo yanatarajiwa kusaidia kuimarisha kazi ya Misioni ya Mungu pamoja na huduma mbalimbali za kijamii.

Kusainiwa kwa makubaliano hayo ni mwendelezo wa ziara ya viongozi na watumishi wa KKKT Dayosisi ya Magharibi Kati waliotembelea KKKT Dayosisi ya Kaskazini kwa muda wa siku sita kuanzia Machi 20, 2026 kwa lengo la kujifunza na kubadilishana uzoefu katika utendaji wa huduma za kanisa.

21/05/2026

AGAPE JUNIOR SEMINARY YATEKELEZA ELIMU AMALI KWA KUJENGA JENGO LA GHOROFA TATU

Katika kuendeleza utekelezaji wa sera ya elimu amali nchini, Agape Lutheran Junior Seminary Secondary School imeanza ujenzi wa jengo la ghorofa tatu litakalotumika kwa shughuli mbalimbali za elimu ikiwemo madarasa ya amali, maktaba ya kisasa pamoja na ukumbi wa matumizi mbalimbali.

Uwekwaji wa jiwe la msingi wa mradi huo ulifanyika wakati wa mahafali ya 25 ya kidato cha sita ya shule hiyo, ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Askofu Dkt. Fredrick Onael Shoo. Jumla ya wanafunzi 67 wamehitimu.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Agape Junior Seminary, Mch. Dkt. Rodrick Limo alisema kuwa mradi huo ni utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 toleo la mwaka 2023 pamoja na mtaala ulioboreshwa unaolenga kutoa elimu bora inayowaandaa wanafunzi kujiajiri, kuajiriwa na kuwa na ujuzi wa ujasiriamali.

Amesema jengo hilo linakadiriwa kugharimu shilingi bilioni moja na milioni mia moja hadi litakapokamilika.

Aidha, walimu na wahitimu wa shule hiyo wameeleza kuwa mafanikio yanayoendelea kupatikana katika shule hiyo yanatokana na nidhamu, juhudi za walimu na wanafunzi pamoja na mazingira bora na rafiki ya kujifunzia yaliyopo shuleni hapo.

Wameeleza kuwa mwaka 2025 waliweza kupata division one kwa wahitimu wote wa kidato cha sita katika mitihani yao ya taifa na kuwa shule ya 7 kitaifa.

18/05/2026

ASKOFU SHOO AWEKA JIWE LA MSINGI NYUMBA YA IBADA MTAA WA SAYUNI

Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Askofu Dkt. Fredrick Onael Shoo, Mei 17, 2026 ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa nyumba ya ibada katika Mtaa wa Sayuni, Usharika wa Pumuani Jimbo la Kilimanjaro Mashariki.

Tendo hilo liliambatana na ibada ya kumstaafisha kwa heshima Mch. Lord Macha, iliyofanyika katika Senta ya Usharika wa Pumuani.

Akisoma risala mbele ya Askofu Shoo, Mchungaji kiongozi wa wa Usharika huo, Danstan Meena, alisema waumini wa Mtaa wa Sayuni wenye jumla ya jumuiya tano walikuwa wakilazimika kusafiri umbali mrefu kufika katika Senta ya Usharika kwa ajili ya ibada.

Alisema hali hiyo ilisababisha baadhi ya waumini kuwa wavivu kushiriki ibada mara kwa mara, jambo lililowasukuma kuanzisha jengo la muda la ibada mwaka 2022 ili kurahisisha huduma za kiroho kwa waumini wa eneo hilo.

Aidha, alisema ujenzi wa jengo jipya la nyumba ya ibada ulianza rasmi Machi 6, 2026, ambapo hadi sasa jumla ya shilingi milioni 27, laki 8 na elfu 50 zimekusanywa kwa ajili ya ujenzi huo.
Mchungaji Meena aliongeza kuwa kukamilika kwa jengo hilo kunatarajiwa kugharimu zaidi ya shilingi milioni 515.

18/05/2026

KATIBU MKUU KKKT DK AELEZA SAFARI YA MAISHA YA UTUMISHI WA MCH. LORD MACHA

Katibu Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Mhandisi Z. S. Moshi, ameeleza safari ya maisha ya utumishi wa Mch. Lord Macha, aliyestaafishwa kwa heshima na Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Askofu Dkt. Fredrick Onael Shoo.

Ibada hiyo ya kustaafishwa ilifanyika katika Usharika wa Pumuani, Jumapili Mei 17, 2026, ambapo viongozi mbalimbali wa Kanisa pamoja na waumini walishiriki kumuaga mtumishi huyo aliyelitumikia Kanisa kwa muda mrefu.

Akizungumza katika ibada hiyo, Mhandisi Moshi alisema kuwa Mch. Macha ametumika katika shamba la Bwana kwa takribani miaka 24 kwa uaminifu, kujituma na moyo wa kujitoa.

Alisema Mch. Macha alikuwa mchungaji aliyempenda Mungu kwa dhati na aliyejitolea kwa hali na mali katika kuwatumikia waumini na kulijenga Kanisa.

Aidha, alimwelezea kuwa alikuwa mtu mwenye misimamo thabiti katika mambo aliyoyaamini kuwa sahihi, huku akijulikana kwa unyenyekevu na ushirikiano mzuri na watu mbalimbali ndani na nje ya Kanisa.

Mhandisi Moshi alisema maisha na utumishi wa Mch. Macha ni mfano wa kuigwa kwa watumishi wengine wa Mungu kutokana na uadilifu, uaminifu na moyo wake wa kujitoa katika kulitumikia Kanisa na jamii kwa ujumla.

17/05/2026

“BE CAREFUL”: ASKOFU DKT. SHOO
Hayo yamesemwa na Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Askofu Dkt. Fredrick Onael Shoo, alipokuwa akihubiri katika Ibada ya Mahafali ya 25 ya Kidato cha Sita katika Seminary ya Agape ya KKKT Dayosisi ya Kaskazini.

Askofu Shoo amesema kuwa kumekuwa na roho ya ukengeufu hasa kwa vijana, hadi kufikia hatua ya kutowasikiliza wazazi na viongozi wao. Amesema kizazi cha sasa kinaonekana kuamini kuwa kinajua kila kitu.

“Wazazi wako wamekulea katika imani thabiti, katika kumcha Mungu na katika mafundisho sahihi ya Bwana. Leo unaona mafundisho hayo ni ya kizamani sana. Muwe waangalifu, roho za udanganyifu zipo,” alisema Askofu Shoo.

Aidha, amesema kuna makundi yanayojulikana k**a “cult”, ambayo huwatoa watu katika imani waliyojengewa na kuwashawishi kumtii kiongozi mmoja anayewatenga na familia, wazazi pamoja na marafiki zao.

“Kundi hilo hukuexploit na kukufanya maskini kabisa. Mwisho wake baadhi ya watu hujikuta katika upweke, na wengine hata kuamua kujiua,” alisema.

Aliongeza kuwa viongozi wa makundi hayo hudai wamepata mafunuo, kisha kuyafanya mafunuo hayo kuwa amri za kuwaendesha waumini wao wanavyotaka.

Askofu Shoo amewataka wahitimu hao kuzingatia malezi na mafundisho waliyoyapata katika seminari hiyo, akisema yatasaidia kupambanua mitego ya shetani na kuishi katika msingi imara wa imani.

15/05/2026

SEMINA YA SIKU NNE YAJADILI SULUHISHO LA UKATILI WA KIJINSIA

Kwa takribani siku nne sasa, semina iliyowakutanisha wasaidizi wa sheria (Paralegal), watoa huduma za mikopo midogo midogo pamoja na viongozi wa dini imeendelea kufanyika kwa lengo la kujadili na kutafuta suluhisho la changamoto ya ukatili wa kijinsia katika jamii.

Semina hiyo inayodhaminiwa na KKKT Dayosisi ya Kaskazini kwa kushirikiana na Norwegian Church Aid imeandaliwa mahsusi kutoa elimu, kuongeza uelewa na kuimarisha ushirikiano kati ya wadau mbalimbali katika mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Washiriki wa semina hiyo wamejadili namna bora ya kutoa msaada wa kisheria kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia, umuhimu wa uwezeshaji wa kiuchumi kwa wanawake na makundi yaliyo hatarini pamoja na nafasi ya viongozi wa dini katika kuelimisha jamii kuhusu madhara ya vitendo hivyo.

Aidha, imeelezwa kuwa ushirikiano kati ya taasisi za dini, watoa huduma za kifedha na wasaidizi wa sheria ni muhimu katika kuhakikisha waathirika wanapata haki zao na jamii inaendelea kuwa salama.

Waandaaji wa semina hiyo wameeleza kuwa mafunzo hayo yatasaidia kujenga jamii yenye uelewa zaidi kuhusu haki za binadamu na kupunguza matukio ya ukatili wa kijinsia yanayoendelea kujitokeza katika maeneo mbalimbali.

13/05/2026

ASKOFU SHOO: KUOMBA KUSIWE KWA KUPAYUKA-PAYUKA

Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dayosisi ya Kaskazini, Askofu Dkt. Fredrick Onael Shoo, amewataka waumini kuwa wanyenyekevu wanapomwomba Mungu na kuepuka tabia ya kuomba kwa kupayuka-payuka au kwa mazoea.

Akihubiri katika ibada ya Jumapili Mei 11, 2026, iliyofanyika Usharika wa Longuo, Askofu Shoo alisema waumini wengi wamezoea kuomba haraka haraka bila kutafakari maana ya sala wanazoziomba, jambo ambalo linapunguza uzito wa mawasiliano yao na Mungu.

Alisema hata Sala ya Bwana haipaswi kuombwa kwa mazoea, bali kwa utulivu na unyenyekevu huku mtu akitambua kuwa anazungumza na Baba wa mbinguni.

“Baba Yetu uliye Mbinguni hatupaswi kuiomba kwa mazoea. Tulia, mtazame Mungu kwamba unazungumza na Baba yako aliye mbinguni. Usiseme tu kwa sababu ni tabia, wengine tunasema haraka haraka tunamaliza. Hapana! Ni sala ambayo imebeba mambo mengi makubwa,” alisema Askofu Shoo.

Aidha, aliwataka waumini kujenga tabia ya kutafakari wanapoomba ili sala zao ziwe na maana na kuleta ukaribu zaidi kati yao na Mungu.

12/05/2026

ASKOFU DKT. SHOO: KANISA LETU LIMEJENGWA KATIKA MSINGI WA NENO LA MUNGU NA MAOMBI.

Askofu Dkt. Fredrick Onael Shoo amesema Kanisa la Kilutheri na walutheri kwa ujumla ni watu wa maombi. Akihubiri kwenye ibada ya Jumapili Mei 11, 2026 Usharika wa Longuo, amesema maombi na Sala ni muhimu sana katika maisha ya kila Mkristo kwa sababu maombi ndiyo njia ya kuwasiliana na Mungu na kufikisha mahitaji yetu kwake kwa sababu yeye ndiye mpaji wetu. "Ili tuweze kusimama katika Imani, tuweze kufanikiwa na kushinda katika maisha haya, tunahitaji kuzungumzia na baba yetu kila wakati". Anaeleza Askofu Shoo Anasema tunapomwomba Mungu, sio kwamba hajui haja zetu bali anapenda tuzungumze naye Kila siku.

11/05/2026

KATIBU MKUU WA KKKT DAYOSISI YA KASKAZINI AFUNGUA SEMINA YA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA MOSHI

Katibu Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Mhandisi Z.S. Moshi, leo Mei 11, 2026 amefungua semina ya siku nne inayowakutanisha viongozi wa Paralegal, Vikoba na Interfaith kutoka dini mbalimbali mkoani Kilimanjaro kwa lengo la kujadili masuala ya ukatili wa kijinsia.

Semina hiyo inayofanyika katika Uhuru Lutheran Hotel & Conference Centre imelenga kujadili changamoto ya ukatili wa kijinsia pamoja na kutafuta njia za pamoja za kupambana na vitendo hivyo vinavyoendelea kuathiri jamii.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa semina hiyo, Mhandisi Moshi amesema kuwa ukatili wa kijinsia ni suala mtambuka lisilochagua dini wala kundi la kijamii, hivyo kuna umuhimu wa wadau mbalimbali kushirikiana katika kuhakikisha vitendo hivyo vinakomeshwa.

“Matukio ya ukatili yamekuwa yakisikika mara kwa mara kupitia vyombo vya habari, hali ambayo inaonyesha ukubwa wa tatizo hili katika jamii yetu. Ni muhimu kujadili chanzo chake na kuona namna ya kushirikiana na Serikali katika mapambano dhidi ya ukatili,” amesema Mhandisi Moshi.

Aidha, amewataka washiriki wa semina hiyo kutumia nafasi hiyo kujadili kwa kina mbinu mbalimbali zitakazosaidia kutoa elimu kwa jamii na kuimarisha ushirikiano baina ya taasisi za dini, viongozi wa jamii pamoja na Serikali.

Semina hiyo imeratibiwa na KKKT Dayosisi ya Kaskazini kupitia Idara ya Uwakili kwa kushirikiana na mradi wa Norwegian Church Aid (NCA), unaoongozwa na Mchungaji Andrew Munisi.

Address

P. O Box 195
Moshi

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when UMOJA DAIMA MEDIA posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Place Of Worship

Send a message to UMOJA DAIMA MEDIA:

Share