31/05/2026
HARAMBEE YA UJENZI WA NYUMBA YA IBADA KILIMA MOJA, MILIONI 127 ZAPATIKANA
Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Askofu Dkt. Fredrick Onael Shoo, leo Mei 31, 2026 ameongoza harambee ya ujenzi wa Nyumba ya Ibada katika Usharika wa Kilima Moja Mtaa wa Kibaoni-Ebenezer, Jimbo la Karatu.
Katika ibada hiyo, Askofu Shoo alimshukuru Mungu kwa kuwakutanisha waumini kuabudu pamoja na kuwapongeza viongozi na washirika kwa hatua nzuri iliyofikiwa ya ujenzi
Akihubiri katika Siku ya Utatu Mtakatifu, Askofu Shoo alimtaja Nehemia k**a mfano wa ujasiri na imani katika kutekeleza kazi ya Mungu licha ya vikwazo. Alisisitiza kuwa ujenzi wa Nyumba ya Mungu ni jukumu la waumini wote na kwamba kila mmoja anapaswa kuchangia kwa uwezo wake, kwa hiari na kwa furaha.
Aliwahimiza waumini kutokata tamaa wala kusikiliza maneno ya kukatisha tamaa, akieleza kuwa kazi inayosindikizwa na maombi haiwezi kushindwa. Pia alisisitiza umuhimu wa umoja, akisema kuwa umoja ndiyo siri ya mafanikio katika kazi ya Mungu.
Askofu Shoo aliwataka waumini kuendelea kushiriki kwa fedha, nguvu kazi na maombi ili kuhakikisha ujenzi huo unakamilika kwa utukufu wa Mungu. Alimalizia kwa kuwakumbusha kuwa kwa Mungu hakuna lisilowezekana.
Mchungaji Kiongozi wa Usharika huo, Goodluck Kwayu, katika risala yake, amesema kuwa ziara ya leo ya Askofu Shoo ni ya kihistoria, akiifananisha na huduma aliyopewa Nehemia ya kusimamia ujenzi wa nyumba ya Mungu.
Amesema Askofu Shoo ameona uhitaji uliopo katika Usharika wa Kilimamoja na kwamba umoja na ushirikiano vitasaidia kutimiza agizo la Yesu Kristo la kufanya mataifa yote kuwa wanafunzi wake.
Mchungaji Kwayu ameeleza kuwa ujenzi wa hekalu umefikia hatua ya sasa kutokana na mchango wa waumini wachache pamoja na marafiki wa usharika. Amesema hatua inayofuata ni upauzi wa jengo, ambao unatarajiwa kugharimu shilingi milioni 62.
Aidha, amesema harambee ya leo inalenga kukusanya jumla ya shilingi milioni 192 kwa ajili ya kukamilisha miradi mbalimbali ya maendeleo katika Usharika wa Kilimamoja. Kipaumbele kikubwa ni kukusanya zaidi ya shilingi milioni 62 kwa ajili ya upauzi wa jengo la mtaa wa Kibaoni–Ebenezer, ambao ndio mtaa pekee ambao jengo lake bado halijapauliwa.