28/07/2026
*UAMINIFU wa THAMANI*
“Baada ya siku nyingi akaja bwana wa watumwa wale, akafanya hesabu nao. Akaja yule aliyepokea talanta tano, akaleta talanta nyingine tano, akisema, Bwana, uliweka kwangu talanta tano; tazama, talanta nyingine tano nilizopata faida. Bwana wake akamwambia, Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako” (Mathayo 25:19-21).
Neno uaminifu ni hali ya mtu kutenda jambo fulani kwa namna ambayo mtu mwingine atamwamini. Kwa lugha nyingine, uaminifu ni HALI ya moyo ambayo itampelekea mtu kuthamini NA kutii utaratibu au jambo la mtu mwingine, “hata k**a hapati faida binafsi” ila anafanya kwa ajili ya mwingine.
Kila nisomapo huu mfano wa talanta najikuta napata somo jipya. Huyu bwana aliporudi “baada ya siku nyingi”, (inamaana hakuwepo hawa jamaa wakifanya kazi), alitoa ZAWADI au alimpandisha cheo huyu jamaa wa talanta 5 aliyezalisha 5 zingine. Angalia tena hapa “Bwana wake akamwambia, Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako”. Huyu mtumwa alikuwa na sifa 2, kwanza ni WEMA, na pili ni UAMINIFU. Angalia tena hapa, bwana wake akarudia tena neno “uaminifu” na kusema ” ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako”! Ina maana kilichomvutia sana bwana wake na kuona huyu jamaa amestahili KUPANDA cheo ni UAMINIFU! Ukiangalia yaliyo msibu yule jamaa wa talanta 1 utagundua aliitwa “MWOVU”, japo kwa mtizamo wa kawaida, alikuwa “mwaminifu” kutunza kilicho cha bwana wake! Sasa angalia hapa, huyu wa talanta 5 alifanya KAZI akaleta FAIDA, huyu wa talanta 1 hakufanya KAZI, “hakupoteza hela ya watu (mtaji) ila pia hakuleta faida”! Akaadhibiwa.
Unapofanya JAMBO la faida (kuzaa matunda), kwa KUAMUA kwa uhuru wako bila kusimamiwa au watu kuona, hilo ni jambo KUBWA! Hawa jamaa wote hawakusimamiwa, bwana wao alisafiri; baada ya SIKU NYINGI alirudi kufanya hesabu. Najaribu kuwaza k**a huyu mtumwa aliyepewa talanta 1 angesimamiwa ingekuwaje? Nashawishika kujibu kwamba “angezalisha pia”, ila sio kwa “kuamua mwenyewe”! Kuna “uaminifu wa thamani” na “uaminifu wa sababu”. Watu wengi ni waaminifu kwa sababu fulani, ila k**a wangekuwa mahali peke yao, wangefanya tofauti! Ni kwa sababu tu “mtu fulani” yupo ndio maana ulijizuia kufanya jambo fulani! Huu ni uaminifu pia ila SIO wa thamni mbele za Mungu.
Nitakupa mfano. Umewahi kufikiri ni watu wangapi wengeenda mbali kabisa na wake/waume zao halafu wakasimama waaminifu? Girl/boyfriends maana hawana la kujitetea pia, wanahusika. Nazungumzia watu ambao “imewapasa” kuishi maisha masafi ila UAMINIFU ni jambo zito. Hebu fikiri mtu anajisifia kwamba mimi sitaanguka katika zinaa/uzinzi, na anawashangaa na “kuwasema” wenzake wakianguka badala ya kuwaombea. Subiri kujaribiwa kuna kuja, kaa sawa. Ghafla! mume/mke anapata shule nje ya nchi, hujakaa sawa mijamaa/wadada wanaanza kuku-beep, hujakaa sawa unaanza kupita vipindi vigumu, wanaokuja kukusaidia ni wale wa jinsia tofauti na wewe, ghafla! tu. Unagundua uko mbali na hakuna “ushahidi”, unaamua kuchukua hatua ngumu za kuvunja UAMINIFU kwa mwenzako na kwa Mungu. Sawa utatubu, utajikausha. Mwenzako akirudi, unaanza kuchachamaa tena, unashambulia wengine walioanguka, unakuwa moto moto na kweli huanguki tena, ila Mungu akiangalia anagundua jambo. Uaminifu wako ni kwa mumeo/mkeo na sio kwa Mungu, maana “bwana wako alipokawia hukuweza kuwa mwaminifu”! Bwana anakupita, hupandi cheo. Mungu akiangalia anaona unafiki tu. Angalia tena uaminifu “ulio wa thamani” maana yake. Wakati hakuna mtu anakuona, unafanyaje?
Vijana wengi wamejifariji kwamba wakioa/olewa wataweza kuwa “waaminifu”. Jua neno hili, ukiweza kuwa mwaminifu sasa, ni ishara kwamba hata kuko mbele utakuwa mwaminifu; ukishindwa kuwa mwaminifu sasa, hata ukioa/olewa unaweza pia ukashindwa kuwa mwaminifu. Zingatia neno hili, ukiwa peke yako (single) na ukawa mwaminifu, huo uaminifu wako ni wa THAMANI sana mbele za Mungu kuliko uaminifu “kwa sababu” umeoa/olewa. Siku hizi utasikia vijana wanapiga mahesamu ya kuoa/olewa ili kushinda tamaa za mwili; baada ya kuoa wanagundua tamaa za mwili na majaribu ya ngozo yameongeka maradufu! Kumbe ulipaswa KUSHINDA ukiwa peke yako ndiposa ushindi huwa dhahiri, kwamba hata sasa baada ya kuoa/olewa unashinda kwa sababu ya Bwana, na sio aibu au hofu ya mwanadamu mwenzio. Kushinda dhambi kwa sababu ya “hofu ya Mungu” ni tofauti na kushinda dhambi hiyo hiyo kwa sababu ya “hofu ya watu”. Thamani za ushindi hizi mbili ni tofauti pia.
Hili jambo la kukosa uaminifu ukiwa peke yako limedidimiza uchumi wa watu wengi. Mungu ameweka vitu “vichache” mkononi mwako, kisha akakaa mbali kuangalia utafanyaje. Ukamsahau Mungu na watu wengine, ukujipendelea kwa sababu uko peke yako na maamuzi yako! Nitakupa mfano mwingine. Umekaa katika nafasi ya maamuzi katika ofisi fulani. Hela zinapita hapo usoni kabisa, unafika mahali unachomoa kidogo na kuweka mfukoni, huku unajifariji eti “kila mtu anafanya hivyo”. Ghafla! Bwana (Yesu) anakuja kukagua mahesabu (moyoni mwako) ili aweze kukuinua katika kiwango kingine cha baraka. Ghafla! anagundua hakuna UAMINIFU, Bwana anapita. Unabaki hapo ukishangaa. Wakati unalalamika na kuonea wengine wivu wakiinuliwa, Roho Mtakatifu anakuonyesha moyo wako, unajua kabisa hata ile hatua uliyovuka ilikuwa sio baraka ya Mungu ila ulicheza faul mahali, unajua, na hilo ndio JIBU Mungu atakujibu ukiomba baraka, Atakufunulia moyo wako uone “mahali ulipoanguka ili utubu” ili akuinue tena. Nakwambia neno hili, ukivushwa na Mungu utajua ni Mungu, ukicheza rafu utajua ni rafu, Roho Mtakatifu hatakaa kimya, utajua tu. Uaminifu wa thamani. Unafanya nini ukiwa peke yako!