27/10/2017
Kisa cha Nabii Ayyubu:
Ni somo kwa Wagonjwa, Wafiwa na waliofilisika!
Ibn Is-haaq amesema kuwa Ayyubu alikuwa ni mtu wa Urumi. Jina lake kamili lilikuwa ni Ayyub bin Musa bin Razih bin Esau bin Ishaaq bin Ibrahim. Mtu mwingine naye akasema, Ayyubu alikuwa akiitwa Ayyub bin Musa bin Rimil bin Esau bin Ishaaq.
Kumekuwa na maelezo mengine kuhusiana na nasaba yake. Ibn Asakir kasimulia kuwa mamaake Ayubu alikuwa ni binti wa Nabii Lut alayhis salam. Ikasemekana pia kuwa babaake Ayyub alikuwa ni mmoja wa wale waliomwamini Ibrahim pale alipotoswa kwenye moto.
Rai ya kwanza ndiyo inayokubalika zaidi kwa sababu Ayyubu alikuwa ni kizazi cha Ibrahim k**a Mwenyezi Mungu alivyosema katika Qur’an, Sura ya 6, aya ya 83-84.
Mwenyezi Mungu, Malaika wamsifu Ayyubu
Mwenyezi Mungu alimsifu mja Wake, Ayyub, “Bila shaka Tulimkuta ni mwenye subira, mja mwema; kwa hakika alikuwa ni mnyenyekevu sana.” (38:44)
Ayyubu alikuwa mwingi wa kuomba toba, mwingi wa kumkumbuka Mwenyezi Mungu, mwingi wa subira na mwenye istiqama. Hii ndiyo sababu ya kupata kwake nusra na ndiyo siri ya kusifiwa hivyo na Mwenyezi Mungu.
Malaika walikuwa katika kundi lao wakiwazungumzia viumbe wengine. Katika maongezi yao, waliwazungumzia waja wanyenyekevu jinsi walivyopata radhi za Mola wao, na wakawazungumzia wale waliotakabari jinsi walivyoghadhibikiwa na Mola wao.
Mmoja wa Malaika hao akasema: “kiumbe bora kabisa duniani hivi leo ni Ayyubu, mtu mwenye tabia njema ambaye kaonesha subira kubwa, na muda wote anamkumbuka Mola wake Mwingi wa Ukarimu. Ni mfano bora wa wenye kumwabudu Mwenyezi Mungu.
Malipo yake, Mola wake kamjaalia uhai mrefu, watoto wengi, na kamneemesha fungu la wenye kuhitaji na masikini. Anawalisha na kuwavisha masikini, na anawanunua watumwa na kuwaachia huru.
Kwa ukarimu na upole wake, anafanya wale wanaopokea zaka kwake wajione k**a vile wao ndio wanaomfanyia fadhila yeye.”
Ibilisi achukizwa na Maneno ya Malaika, Amwandama Ayyubu!
Ibilisi aliposikia yote hayo yaliyosemwa na Malaika katika kumsifu Ayyubu, akachukizwa. Akajipanga kumyumbisha Ayyubu ili aharibikiwe na kukufuru, basi akamwendea haraka.
Alijaribu kumvurugia Sala zake kwa kumnong’oneza mambo mazuri ya kimaisha lakini Ayyubu alikuwa ni muumini kwelikweli na hakuruhusu mawazo mabaya yambabaishe na kumvurugia Sala zake.
Jambo hilo likamkera zaidi Ibilisi. Sasa akaanza kujenga chuki mbaya sana dhidi ya Ayyubu. Ibilisi akalalamika kwa Mwenyezi Mungu kuhusu Ayyubu.
Akasema kuwa japo muda wote Ayyub alikuwa anamtukuza Mwenyezi Mungu lakini alikuwa akifanya hivyo bila ikhilasi ila kumpoza tu Mungu ili utajiri wake usiondoshwe. Akasema, ni riya tu aliyofanya Ayyubu, na hiyo ni kutokana na tamaa ya mali.. “Ukimuondoshea utajiri, utaona kuwa ulimi wake hautalitaja tena Jina lako na sala zake zitaishia hapo.”
Mwenyezi Mungu akamwambia Ibilisi kuwa Ayyubu alikuwa ni mcha Mungu kwelikweli. Hakumwabudu Yeye eti kwa sababu ya neema; ibada yake ilitoka moyoni kabisa na haikuhusiana na vitu vya kidunia.
Lakini, ili kumthibitshia Ibilisi kiwango cha ikhilasi na subira ya Ayyubu, Mwenyezi Mungu akamruhusu Ibilisi na wasaidizi wake wafanye chochote walichotaka dhidi ya utajiri wa Ayyubu.
Ibilisi akafurahi sana. Akawakusanya wasaidizi wake, na wakafanya ya kufanya kuhujumu mifugo ya Ayyubu, kuwahujumu watumishi wake na kuhujumu mashamba yake mpaka akabaki mee! Mtupu kabisa.
Baada ya hujuma hiyo, sasa Ibilisi akajitokeza kwa Ayyub akiwa k**a mzee fulani hivi wa kibinadamu mwenye busara zake, na kumwambia:
“Bwana wewe Utajiri wote umekutoweka, eti baadhi ya watu wanasema kuwa ulizidi sana kutoa-toa sadaka na unapoteza bure muda wako kwa kuswali-swali muda wote. Wengine wanasema eti Mungu kakukomoa ili awafurahishe maadui zako. K**a Mungu ndiye Mwenye uweza wa kukinga hasara, si basi angekukingia utajiri wako.”
Akiwa mkweli wa imani yake, Ayyub akajibu: “Kile ambacho Mwenyezi Mungu kakichukua kwangu ni mali Yake Yeye Mwenyewe. Mimi nilikuwa mtunza amana wa muda tu. Yeye humneemesha Amtakaye na Humnyima Amtakaye.” Baada ya kusema maneno haya, Ayyubu, kwa mara nyingine, akapomoka kumsujudia Mola wake.
Ibilisi alipoona hivyo, akachanganyikiwa, na hivyo, akamwambia tena Mwenyezi Mungu: “Nimemvua Ayubu mali zote, lakini bado anaendelea kukushukuru. Lakini huyu anaficha tu huzuni yake, kwani kaweka akiba ya watoto wengi alionao. Mtihani halisi wa mzazi ni kwa watoto wake. Utaona jinsi Ayyubu atakavyokukufuru.”
Mungu akampa Ibilisi idhini lakini akamtahadharisha kuwa hiyo haitashusha imani ya Ayyubu kwa Mola wake wala haitampunguzia subira. Ibilisi akakusanya tena wasaidizi wake na kupanga hujuma zake. Akatikisa muhimili wa nyumba ambayo watoto wa Ayyubu walikuwa wakiishi na kusababisha jengo liporomoke na kuua watoto wote.
Kisha akaenda kwa Ayyubu kwa kujifanya yeye ni mwanadamu mwema aliyekuja kumfariji. Kwa sauti ya kumfariji, akasema, “Mazingira ambayo watoto wako wamefia yanasikitisha kwa kweli! Mungu hata hakulipi Sala zako sawasawa.” Baada ya kusema hivyo, Ibilisi akasubiri kwa hamu na matumaini kuwa sasa Ayyubu alikuwa tayari kumkufuru Mungu.
Lakini, kwa mara nyingine, Ayyub akamfadhaisha kwa kujibu: “Mwenyezi Mungu, wakati mwingine, hutoa, na wakati mwingine, hutwaa. Wakati mwingine, hufurahishwa na wakati mwingine, huchukizwa na matendo yetu. Mimi, iwe faida, iwe hasara kwangu, nitabaki kushik**ana na imani yangu na nitaendelea kumshukuru Mola wangu.” Baada ya kusema hivyo, Ayyubu akapomoka kumsujudia Mola wake. Ibilisi akakerwa mno na jambo hilo.
Ibilisi akamuomba Mungu: “Ewe Mola wangu! Mali ya Ayyubu imekwenda, watoto wamekufa, naye bado ana afya nzuri ya kiwiliwili. Maadam ana afya nzuri, ataendelea kukuabudu kwa matumaini ya kupata tena utajiri na kuzaa watoto zaidi, Nipe idhini juu ya kiwiliwili chake ili nikidhoofishe. Kwa hakika ataacha kukuabudu na hivyo atakuwa muasi.”
Mwenyezi Mungu akataka kumpa somo Ibilisi kwamba Ayyub alikuwa mja mchaMungu basi akamkubalia ombi lake la tatu lakini akamwekea sharti hili: Nakupa idhini juu ya mwili wake lakini sio roho yake, akili yake wala moyo wake, kwani humu ndimo inamokaa Ilimu yangu na dini Yangu.”
Akiwa amepata idhini hii mpya, Ibilisi akaanza mashambulizi ya kulipiza kisasi dhidi ya kiwiliwili cha Ayyubu, na akakijaza maradhi hadi kikakondeana na kubaki ngozi na mifupa mitupu huku akiugulia maumivu kadha wa kadha.
Lakini katika kipindi chote cha kuugulia, Ayyub alibaki na nguvu ya imani. Kwa subira ya hali ya juu, alihimili masaibu yote bila kulalamika, kusononeka.
Mja huyu mwema wa Mwenyezi Mungu hakukata tamaa wala hakuwaelekea wengine kuomba msaada, bali yeye alibaki kutumainia rehema za Mwenyezi Mungu. Ikafika mahala hata ndugu na jamaa wa karibu nao wakamtupa kabisa.
Ni mkewe pekee aliyebaki naye kwa huruma na mapenzi. Katika kipindi cha matatizo, mke huyu akaonesha huruma kwa mumewe na kumuuguza. Ndiye mwenza na mfariji pekee aliyebaki naye katika miaka mingi ya kuugua.
Ibn Asakir kasimulia: “Ayyubu alikuwa na mali za aina zote, watumishi, kondoo, mashamba makubwa ya Haran na watoto wengi. Neema zote hizo zikaondoshwa kwake, na akakumbwa na maradhi ya mwili.
Hakukuwa na hata kiungo kimoja kilichokuwa na afya isipokuwa moyo na ulimi, huku akitumia vyote viwili kumtukuza Mwenyezi Mungu, usiku na mchana. Maradhi yalimchukua muda mrefu hadi wageni waliokuwa wakimtembelea (kumjulia hali) wakachoka naye.
Rafiki zake wakajitenga naye, na watu wakaacha kumtembelea. Hakuna aliyemfariji isipokuwa mkewe. Akamuhudumia mumewe vizuri, akikumbuka fadhila na huruma ya mumewe kwake siku za nyuma.”
Basi Ibilisi akawa na hali ngumu. Akashauriana na wasaidizi wake, lakini hawakuweza kumshauri. Wakamuuliza: “inakuwaje ujanja wako unashindwa kufanya kazi kwa Ayyubu ilihali ulifanikiwa kumpoteza Adam, baba wa wanadamu, na kumtoa Peponi?”
Ibilisi akaenda kwa mke wa Ayyubu kwa sura ya mwanaume wa kibinadamu. Akajidai kuuliza: “Mumeo yuko wapi?” Mke wa Ayyubu akaonesha kiwiliwili ambacho aghalabu kilikuwa k**a mfu, chakachaka kabisa kitandani na kusema: “Yule pale, anapembea baina ya uhai na kifo.”
Ili kumuumiza kihisia na kumtia uchungu, Ibilisi akamkumbusha mke wa Ayyubu enzi za afya nzuri ya mumewe, enzi zao walipokuwa na mali na watoto. Tahamaki kumbukumbu ya uchungu ya miaka ya matatizo ikamzidia mke wa Ayyubu, na akaanza kububujikwa na machozi.
Akamwambia Ayubu, “(Mume wangu)! Hadi lini utaendelea kuvumilia mateso haya kutoka kwa Mola wako? Je, ndio basi jamani tubakie hivi hivi, moja kwa moja bila mali, watoto wala jamaa? Kwa nini usimuombe Mwenyezi Mungu atuondoshee machungu haya jamani?”
Ayyubu akavuta pumzi, na kwa sauti ya mbali ya mgonjwa aliye taabani, akajibu: “Ni Ibilisi tu huyo ambaye atakuwa amekuchochea wewe na kukufanya usononeke namna hiyo! Hebu niambie (mke wangu), ni kitambo gani mie nilifurahia afya njema na utajiri?
Mkewe akajibu: “miaka 80
Kisha Ayyubu akasema, “Nina muda gani tangu nilipoanza kuugua?
Mkewe akajibu: miaka 7
Ayyubu akamwambia mkewe: “Basi, k**a ndio hivyo (mke wangu), mimi mwenzio naona aibu kumuomba Mola wangu aniondoshee shida, kwani mbona sijataabika muda mrefu kulinganisha na miaka mingi ya afya njema na utajiri! Inaonekana wewe mwenzangu imani yako imedhoofu na huridhiki na Qadari ya Mwenyezi Mungu.
Nikipona mie wewe, naapa n’takuchapa mie, fimbo mia! Tena kuanzia leo sitaki tena kula au kunywa chochote mkononi mwako. Basi niache tu peke yangu, na mwache Mola wangu anifanyie chochote akipendacho.”
Akilia kwa uchungu na kwa moyo mzito wa huzuni na huruma (kwa mumewe), mke wa Ayyubu hakuwa na namna isipokuwa kuondoka na kwenda kutafuta mahali pengine pa kuishi. Huyu ni mtu wa mwisho tena, sasa Ayyubu kabaki peke yake, nani wa kumlisha, nani wa kumywesha, nani wa kumgeuza ubavu kitandani?
Katika hali hiyo ya kukosa kabisa msaada, Ayyubu akamuelekea Mola wake, sio kulalamika bali kuomba rehema Zake.
“Na (mtaje) Ayyubu alipomwita Mola wake (akasema): “Mimi imenipata dhara, Nawe ndiwe Unayerehemu kuliko wote wanaorehemu. Basi Tukamkubalia (wito wake) na Tukamuondolea dhara aliyokuwa nayo. Na Tukampa watu wake na mfano wao pamoja nao.
Ni rehema inayotoka Kwetu, na, ni ukumbusho kwa wafanyao ibada” (21:83-84)
“Na mkumbuke mja Wetu Ayubu, alipomwita Mola wake, “Kwa yakini Shetani amenifikishia udhia na taabu. (Niondoshee Mola wangu maradhi haya yaliyonifika). (Mwenyezi Mungu akamwambia), “Uharakishe mguu wako (patachimbika chemchem chini yake, maji yake yatakuwa dawa yako. Basi haya maji baridi ya kuoga, na ya kunywa. Na Tukampa watu wake na wengine k**a wao pamoja nao, kwa rehema itokayo Kwetu, na (ipate kuwa) mauidha kwa wenye akili.” (38:41-43)
Ayyubu alifanya hivyo, na papo hapo, afya yake nzuri ikarejea. Wakati huo huo mkewe naye kule alikokuwa huruma ilimja kwa hali aliyomuacha nayo mumewe. Akashindwa kuendelea kukaa mbali na mumewe na akarejea ili kuomba msamaha na kuendelea kumuhudumia.
Alipoingia ndani ya nyumba, akashangaa kuona mabadiliko ya ghafla: Ayubu alikuwa bukheri wa afya k**a zamani! Akamkumbatia na kumshukuru Mwenyezi Mungu.”
Ayyubu alikuwa amekula kiapo cha kumwadhibu mkewe k**a angepata afya, lakini sasa hakutaka tena kumuumiza mkewe. Alijua kuwa k**a asingetimiza kiapo chake, basi angekuwa na hatia ya kuvunja ahadi yake kwa Mwenyezi Mungu.
Kwa sababu hiyo, Mwenyezi Mungu, kwa Hikima na Rehema Zake zisizo na ukomo, akamsaidia mja Wake huyu mwema na akamnasihi hivi:
“Na kisha shika kicha cha vijiti tu mkononi mwako (si fimbo), kisha mpige kwacho mkeo, wala usivunje kiapo.” (38:44).
IJUMAA MUBARAK