11/07/2020
SOMO: USIOGOPE MWAMINI YESU
Hofu nini?
Hofu ni hisia inayosababishwa na hatari au tishio.
Hofu huanzia kwenye ubongo baada ya kupata taarifa ya hatari au tishio kupitia milango mitano ya fahamu: yaani kuona, kusikia, kunusa, kuonja na kugusa. Mwitikio huu wa hofu huenea mwili mzima.
Hisia hizi zina nguvu sana, husababisha athari mbaya za kiakili, kimwili na kiroho.
Kiakili:- Hofu inamwondolea mtu utulivu wa mawazo, umakini na busara ya maamzi mazuri. Mtu anaweza kukimbia hovyo, kujificha na kufeli masomo katika mitihani.
Kimwili:- Hofu inasababisha maumivu ya kifua au tumbo, midomo kukauka, kichefuchefu, mapigo ya moyo kwenda mbio, kupumua kwa shida, kutetemeka, kukosa usingizi nk
Kiroho:- Hofu inasababisha mtu kusahau ahadi za Mungu, matendo makuu aliyotendewa na mwisho kupoteza kabisa imani kwa Mungu.
Vyanzo vya hofu ni vingi sana kutegemea mhusika na mazingira yake. Hatari na matisho yanaweza yakalenga: afya, familia, uchumi, masomo, hatima ya maisha nk. Mungu anajua mapito yako na yupo karibu nawe akusaidie.
Bwana Yesu anasema hivi katika (Yn 14:1) Msifadhaike mioyoni mwenu; mwaminini Mungu, niaminini na mimi. Jibu la hofu zako ni kumwamini Mungu katika Jina la Yesu. Mungu ndiya msaada wa kweli katika hatari na majanga ya aina zote .Kwa sababu Mungu mwenyewe ameahidi katika Neno lake anasema:-
Kwa maana mimi, Bwana, Mungu wako, nitakushika mkono wako wa kuume, nikikuambia, Usiogope; mimi nitakusaidia. (Isaya 41: 13)
Bwana, aliyekufanya, na kukuumba toka tumboni, yeye atakayekusaidia, asema hivi; Usiogope, ... (Isaya 44: 2)
Mpendwa msomaji wangu, unapopita katika majaribu mazito, usiogope maana Mungu yupo kukusaidia. Haijalishi ukubwa wa jaribu wala uhalisia wa madhra yanayoweza kutokea.
Nimekwambia hofu huanzia kwenye ubongo, unaweza kuona au kusikia maafa makubwa yaliyotokea mahali fulani yakakuogopesha na kupoteza imani. Mfano covid 19 ilipolipuka ilitikisa dunia na kuua watu wengi sana katika nchi zilizoendelea tofauti na Tanzania nchi changa kiuchumi, kitekinolojia na hata kiutaalam. Ukweli corona iliingia Tanzania lakini madhara yake hayakuwa makubwa k**a ilidhaniwa na shirika la afya la dunia WHO. Siri yake ni nini?
Mheshimiwa rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania alilitia moyo taifa letu lisiogope corona kupitiliza na alipiga mbiu ya maombi ya kitaifa ya siku tatu. Alisisitiza imani kwa Mungu zaidi ya dawa madaktari na barakoa, bila kupuuza tahadhari za wataalamu wa afya.
Tunamshukuru Mungu aliyeingilia kati kuliponya taifa letu la Tanzania na covid 19 ikiwa ni matokeo ya majibu ya maombi yaliyofanyika nchi nzima na baadhi ya madhehebu yaliendelea kuliombea taifa bila kukoma. Mataifa ya ya nje yanaishangaa Tanzania kulikoni ? Jibu kuna Mungu aliyesikia maombi ya watanzania waliyoomba kwa imani bila hofu wala mashaka.
Ahadi za Mungu ni kweli, tukilishika Neno na kufanya maagizo yake anatuponya kabisa.
Ee nchi, usiogope; furahi na kushangilia; kwa kuwa Bwana ametenda mambo makuu. (Yoel 2: 21)
Akawaambia, Kwamba utaisikiza kwa bidii sauti ya Bwana, Mungu wako, na kuyafanya yaliyoelekea mbele zake, na kutega masikio usikie maagizo yake, na kuzishika amri zake, mimi sitatia juu yako maradhi yo yote niliyowatia Wamisri; kwa kuwa Mimi ndimi Bwana nikuponyaye. (Kutoka 15:26)
Mpendwa wangu, katika matatizo yako magumu ya kutisha, usiogope, sikiliza Neno lake, tenda maagizo yake na umwamini Yesu Kristo kwa kumaanisha kuwa yeye ni mwokozi hutaangamia. Neno la Mungu linakwambia:-
Kwa kuwa amekaza kunipenda Nitamwokoa; na kumweka palipo juu, Kwa kuwa amenijua Jina langu. Ataniita nami nitamwitikia; Nitakuwa pamoja naye taabuni, Nitamwokoa na kumtukuza. ( Zaburi 91:14-15) Tena anasema
Naye Bwana, yeye ndiye atakayekutangulia, atakuwa pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha; usiogope wala usifadhaike. (K*m 31:8)
Kwa ahadi za uhakika namna hii unayo sababu gani ya kuogopa? Kwa nini umwache Mungu, ujiingize kwenye ushirikina ukidhani utapata msaada kwa waganga wa kienyeji?. Unapopita katika nyakati ngumu ni vita, usipokuwa jasiri utashindwa. Mungu anasema:-
Je! Si mimi niliyekuamuru? Uwe hodari na moyo wa ushujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako. (Yos 1: 9)
Mungu ni msaada wako wa karibu, unaopatika tele wakati wa mateso. Mwite atakuitikia. Mtwishe mizigo yako atakuchukulia na umwamini katika vita vyako atakupigania. Anapenda kukuona unaishi maisha ya amani na utulivu ndiyo sababu ya Yesu kuja duniani. Ubarikiwe.
Rev. F. M. Swenya
Wasiliana nami: 0767 469 595/0784 469 595/0673 469 585