29/12/2025
HERI YA MWAKA MPYA 2026 TUNAOUTARAJIA, TUKIJALIWA.
Wakolosai 3:23-24.
Tulichokianzisha kwa gharama kubwa tutakilea kwa dhamira kubwa. Tutafanya hivi tukijua kwamba kuanzisha jambo kubwa ni ujasiri lakini kuliendeleza ni uwajibikaji.
Ndugu zangu, Ujumbe wangu wa Mwaka Mpya tunaoutarajia ni huu:
Hatuanzishi vitu ili baadaye tuje tuviachie vififie na hatimaye kufa kwa kuvitelekeza. K**a hilo lingekuwa lengo letu tangu mwanzo, basi tungejiuliza kwa dhati: Kwa nini tulitumia muda wetu, nguvu zetu, na rasirimali zetu za thamani kuvianzisha? Ukweli ni mmoja—hakuna anayepanda mbegu akiwa na matumaini ya kuvuna majivu.
Tulianzisha haya mambo kwa sababu tuliona thamani yake. Tuliona mustakabali wake. Tuliona namna ambavyo yangeweza kukua, kustawi, na kuwa baraka kwetu sisi na kwa wengine. Ndani ya kila hatua ya mwanzo kulikuwa na ndoto, matumaini, na imani kuwa juhudi zetu hazitakuwa bure.
Changamoto njiani hazipaswi kuwa sababu ya kukata tamaa, bali ziwe kumbusho la kwa nini tulianza. Kila kitu chenye thamani hupitia misukosuko kabla hakijaimarika. Ni wajibu wetu kusimama imara, kurekebisha pale panapohitaji kurekebishwa, na kuendelea kusukuma mbele hata pale panapochosha.
Tusikubali vile tulivyovianzisha kwa gharama kubwa vife kwa sababu ya uzembe, woga, au kukosa umoja. Badala yake, tushikane, tushirikiane, na tuvilee kwa bidii mpya. Kwa kufanya hivyo, si tu kwamba tutavihifadhi, bali tutaviona vikikua na kuleta matunda ambayo yatakuwa fahari yetu sote.
Huu ni wakati wa kuchagua—kuacha au kuendeleza.
Mimi nimechagua kuendeleza. Mwenzangu, ndugu yangu, umechagua lipi?
TWAA TENA! Tawi la Mzabibu Unaozaa!
Hali nikijaa shukrani za neema kwa 2025, nakutakia wewe pamoja nami mwaka 2026 wenye heri na mibaraka ya kushangaza! Amina.
Pastor Innocent Kapenda
Man of Grace