31/05/2026
NJOMBE – Mkutano wa uinjilisti wa Njombe Net Event 2026 wenye kaulimbiu ya “Tumaini Lenye Baraka” umehitimishwa kwa mafanikio makubwa mkoani Njombe, ukisimamiwa na Chama cha ATAPE kwa kushirikiana na Kanisa la Waadventista Wasabato Tanzania.
Katika hitimisho la mkutano huo, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mheshimiwa Antony Mtaka, alikabidhiwa Tuzo na Cheti cha Utambuzi kwa kuthamini mchango wake mkubwa katika kuunga mkono shughuli za kanisa na ushirikiano wake wa karibu na Chama cha ATAPE katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kijamii na kiroho.
Viongozi wa ATAPE walieleza kuwa Mheshimiwa Mtaka ameendelea kuwa mshirika muhimu wa kanisa tangu kuanzishwa kwa mikutano hiyo, jambo ambalo limechangia mafanikio ya shughuli mbalimbali zinazolenga kuleta maendeleo na ustawi wa jamii.
Mkutano huo uliwakutanisha washiriki, viongozi wa dini, wadau na wawezeshaji mbalimbali kwa lengo la kuhubiri injili, kuimarisha maadili na kuhamasisha matumaini kwa wananchi kupitia mafundisho ya kiroho na huduma za kijamii.
ATAPE wametoa shukrani za dhati kwa washiriki wote, wadau, viongozi, wawezeshaji na kila aliyeshiriki kwa namna moja au nyingine kufanikisha mkutano wa Njombe Net Event 2026, wakieleza kuwa mkutano huo umeendelea kuwa chombo muhimu cha kuleta tumaini, mabadiliko chanya na baraka kwa watu wengi katika jamii.