02/06/2026
MASOMO YA MISA, JUMANNE YA JUMA LA TISA, KIPINDI CHA KAWAIDA, MWAKA II, JUNI 2, 2026
RANGI YA KILITURJIA: KIJANI KIBICHI 💚
SOMO LA KWANZA
2 PETRO 3:11b—15a, 17—18
Tunatarajia mbingu mpya na nchi mpya.
Somo katika barua ya pili ya Mtakatifu Petro
Ndugu wapendwa: Je haiwapasi ninyi kuishi kitakatifu zaidi na kumcha Mungu, kungoja na kuukimbilia ujio wa siku ya Mungu, ambapo mbingu zitateketea moto na kutoweka, na viumbe vitayeyushwa kwa mwako wa moto? Kisha tunatazamia - k**a alivyoahidi - mbingu mpya na nchi mpya zenye uadilifu. Mkisubiri hayo, ndugu wapendwa, mjibidishe kuishi bila mawaa ili mkutwe katika amani. Bila shaka, subira ya Bwana wetu inawapatia salama. Lakini, ninyi, ndugu wapendwa, mmeonywa juu ya mambo hayo. Kwa hiyo jihadharini, msije mkachukuIiwa na maoni ya uongo ya wahalifu, kupotewa na uthabiti wenu na kuanguka. Zidini katika neema na ufahamu wa Bwana wetu na mwokozi Yesu Kristo. Utukufu kwake, sasa na hata milele. Amina.
NENO LA BWANA... TUMSHUKURU MUNGU
ZABURI YA KUITIKIZANA
ZABURI 90:2, 3—4, 10, 14 na 16 (K 1)
K. Wewe Bwana, umekuwa kimbilio letu, toka kizazi hata kizazi.
Kabla ya kuzaliwa milima,
na hujaumba dunia au ulimwengu,
toka milele hata milele, wewe upo, ee Mungu. K.
Unamrudisha mtu mavumbini.
ukisema, "Rudini, enyi wanadamu."
Maana miaka elfu machoni pako
ni k**a siku ya jana, iliyokuja na ikapita,
au k**a lindo la usiku. K.
Jumla ya miaka yetu ni sabini.
au tukiwa na afya njema, themanini.
Na mingi ya miaka hiyo ni taabu na shida
Nayo yapita mbio, nasi twatoweka mara. K.
Alfajiri, utushibishe kwa huruma yako:
nasi tutashangilia na kufurahi siku zetu zote.
Matendo yako na yaonekane kwa watumishi wako,
na utukufu wa nguvu yako kwa watoto wao. K.
SHANGILIO LA INJILI
TAZAMA WAEFESO 1:17—18
K. Aleluya. W. Aleluya.
K. Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, ayaangaze macho ya mioyo yetu, ili tupate kujua tumaini la mwito wetu jinsi lilivyo.
W. Aleluya.
SOMO LA INJILI
MARKO 12:13—17
Mpeni Kaisari yaliyo yake Kaisari, na Mungu yaliyo yake Mungu.
†Somo la Injili takatifu ilivyoandikwa na Marko
Wakati ule: Waliwatuma baadhi ya Mafarisayo na watu wa Herode kwa Yesu kusudi wamnase katika kuongea. Nao walimjia, wakamwambia, "Mwalimu, twajua ya kuwa wewe u mwadilifu, tena hufanyi ubaguzi, wala cheo cha mtu si kitu kwako, bali unafundisha njia ya Mungu kwa ukweli tu. Je, ni halali kumlipa Kaisari kodi au sivyo? Tumlipe au tusimlipe?" Naye alitambua unafiki wao, akawaambia, "Mbona mnanijaribu? Nileteeni sarafu niitazame." Wakaileta, naye akawaambia, "Sanamu hii na hati hii ni ya nani?"" Wakamjibu, "Ni ya Kaisari." Yesu akawajibu, "Mpeni Kaisarà yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu." Wakamstaajabia sana.
INJILI YA BWANA... SIFA KWAKO EE KRISTO