26/06/2023
LESONI LEO, JUNI 25-PAULO, MWINJILISTI HUKO EFESO
Katika kazi yake ya Uinjilisti, Paulo anafika Efeso! Moja ya miji mikubwa kabisa ya himaya ya kirumi, moja ya miji tajiri ya himaya ya kirumi, moja ya miji iliyokuwa ikikua na kustawi, mji wa biashara, moja ya miji ambayo watu waliabudu miungu mingi na Artemi (mungu mke) ndiye aliyechukuliwa kuwa mlinzi wa mji huo (Efeso) na alikuwa mkuu zaidi!!!
Huko (Efeso) Paulo anahubiri injili, anatenda miujiza na kuwavuta wengi kwa Kristo! Tazama Matendo 19:1-12. Lakini pamoja na kwamba wengi walivutwa, bado kuna wengi ambao hawakuamini. Lakini maandiko yanatwambia katika Matendo 19, kwamba baada ya muda kadhaa kupita, wengi waliokuwa hawaamini na wale ambao waliamini kidogo (ambao walijisalimisha kidogo kwa Kristo), wote, waliamini na kundi la wakristo katika Efeso likaongezeka!!! Nini basi kilichoongeza kundi?! Nini kilichofanya wale ambao hawakuamini hapo awali wajisalimishe kwa Kristo?! Nini kilichofanya walio nusu nusu, wajitoe kikamilifu kwa Kristo?! 👇
- Luka anasimulia kisa cha ajabu cha Wayahudi saba wapunga pepo, wenye kuzunguka zunguka katika mji, ambao wanachanganya jina la YESU na Paulo katika uchawi wao, kwa lengo la kutenda miujiza. Kuchanganya jina la YESU na mtumishi wake Paulo katika uchawi wao kunaonekana kuwa jambo lisilofaa kabisa na linaloleta madhara kwa Wayahudi hao (Kwani maandiko yanasema hivi baada ya kulichanganya jina la YESU na Paulo katika uchawi wao, pepo waliwarukia na kuwaletea madhara).
Kisa hicho kiliwavuta wengi ambao hawakuamini katika Efeso, na wengi ambao walijitoa nusunusu (baada ya kugundua kwamba) wanapaswa kujitoa kikamilifu, walijitoa kikamilifu kwa YESU na kundi la Kikristo katika Efeso na kicho, vikaongezeka!!! Tazama Matendo 19:13-20.
Nimalizie kwa kusema hivi; Ibada ya YESU, haipaswi kuchanganywa na kitu chochote au mtu mwingine yeyote!!!
TAFAKARI NJEMA SANA....