15/04/2024
IJUE SIRI YA KULA MEMA YA NCHI.
Bwana Yesu asifiwe mtu wa Mungu, ni siku nyingine tena Mungu ametupatia kibali na neema ya kukutana pamoja tukizidi kujifunza habari za uzima.
Somo letu la leo linaenda kukupa mwanga na kukusogeza hatua nyingine kwenye safari yako ya Ukristo.
Ni hitaji la kila mwandamu aliyepo Duniani kuyapata na kuyafurahia Mema ya nchi yaani hakuna anayependezewa au kuhitaji apate mabaya ya nchi. Juhudi na Bidii ya kila mwanadamu ni kuyapata mema ya nchi lakini bahati mbaya ni kwamba wengi wanayahitaji mema ya nchi ila hawajui siri na msingi wa kwanza wa kupata mema ya nchi hivyo leo unaenda kujifunza msingi wa kwanza wa kuyapata Mema ya nchi.
MEMA YA NCHI NI NINI?
Haya ni mambo mazuri ambayo Mungu ameyaandaa kwa ajili ya mwanadamu ayapate pindi tu anapozaliwa na kipindi chake chote cha maisha juu ya Uso wa nchi. Mambo haya mengi ni mahitaji ya msingi na mambo ya muhimu kwa mwanadamu.
Mfano wa Mema ya nchi ni Afya njema, kuishi miaka mingi, hali nzuri ya maisha, mafanikio ya kimwili yaani utajiri na Mali, Ndoa, familia Bora, furaha, amani na mengine Mengi.
YANAPATIKANA VIPI?
Kila mmoja amekuwa na namna yake na msingi wake wa kuyatafuta Mema ya nchi wapo ambao wameamini kuwa bidii ndio msingi wa kuyapata mema ya nchi lakini hawajafanikiwa kuyapata na hata walipolipata moja halikudumu.
Wapo wengine wanahama makanisa kila siku wakitafuta muujiza na siri ya kuyapata mema ya nchi. Kila upepo unaopita umewachukua lakini bado hawajayapata.
Wengine wapo kwenye Maombi miaka Nenda Rudi lakini bado hawajafanikiwa kuyapata waneshangaa pale wanapoona wengine wakiyapata.
Wengine wapo kwa waganga huko, walilipata moja nalo likazaa uchungu na kugeuka kuwa ubaya.
Wengine wapo kwa mitume, wachungaji na manabii wakitafuta upako wakiamini ni michezo ya watu au laana zinawafuata au wamerogwa lakini bado wamejilisha upepo na hakuna matokeo kwao.
NENO LA MUNGU LINASEMA.
Msingi wa kuyapata mema ya nchi upo mmoja pekee na ndio mema yote yanazaliwa hapo hakuna mema ya nchi nje ya msingi huo ambao nabii Isaya ameutaja hapa.
Isaya 1:19-20
[19]Kama mkikubali na kutii mtakula mema ya nchi;
[20]bali k**a mkikataa na kuasi mtaangamizwa kwa upanga; maana kinywa cha BWANA kimenena haya.
anasema
MKIKUBALI KUTII MTAKULA MEMA YA NCHI.
Kumbe UTIIFU ndio msingi wa kwanza wa kula mema ya nchi na huo utiifu ni kumtii MUNGU kwa kulishika na kulitenda NENO LAKE, hii ndio tiketi ya kwanza ya kula mema ya nchi.
Hakuna mema ya nchi yanayopatikana pasipo kumtii na kuyatenda mapenzi ya Mungu kwano hata yakipatikana huleta uharibifu na kuzaa uchungu.
Msingi wa kwanza wa mafanikio yako mwanadamu ni kumtii Mungu na baada ya hapo unaweza kuyapata Mema yote ya nchi uliyoandaliwa na Mungu.
Msingi wa kuwa na ndoa Bora, familia bora, maisha bora, furaha, amani, utajiri na mengine unaanzia kwenye kulishika na kulitenda Neno la Mungu kwanza.
Pasipo kumtii Mungu utafanya bidii na mwisho utafika ukiwa umefanya kazi ya kuchosha usiku kucha pasipo matokeo.
TUNAPATAJE KUMTII MUNGU?
Njia pekee ya kumtii na Kulishika Neno la Mungu ni kwa kumwamini Yesu Kristo k**a Bwana na mwokozi wa maisha yako yaani kumpokea Kristo. Mema ya nchi yamefichwa kwenye kuamini mauti na kufufuka kwake Yesu Kristo.
Ukimuamini Yesu Kristo atakupa nguvu ya kumtii Mungu kwa kulishika na kulitenda Neno lake na kuyapata mema yaliyoandaliwa kwa ajili yako.
Mema ya nchi yanapatikana kwa kumwamini Yesu Kristo ambaye ndani yake imo ahadi ya kuyapokea Mema yote ambayo umeandaliwa kuyapata hapa duniani kwani kwa kila aliyeviacha vyote na kumfuata Yesu ameahidiwa kuvipata.
YESU ANASEMA.
Mathayo 19:27-29
[27]Ndipo Petro akajibu, akamwambia, Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata; tutapata nini basi?
[28]Yesu akawaambia, Amin, nawaambia ya kwamba ninyi mlionifuata mimi, katika ulimwengu mpya, atakapoketi Mwana wa Adamu katika kiti cha utukufu wake, ninyi nanyi mtaketi katika viti kumi na viwili, mkiwahukumu kabila kumi na mbili za Israeli.
[29]Na kila mtu aliyeacha nyumba, au ndugu wa kiume au wa k**e, au baba, au mama, au watoto, au mashamba, kwa ajili ya jina langu, atapokea mara mia, na kuurithi uzima wa milele.
Hakuna ambaye ataviacha vyote kwa ajili ya Yesu Kristo halafu akayapata mabaya ya nchi kwani ndani yake umo ulinzi na tiba za urogaji wote, anaondoa laana na mikosi yote kwa jina lake na huo ndio upako uliopo ndani yake Kristo.
Ndugu Yangu Mkristo kabla hujaanza kufanya bidii kuyatafuta mema ya nchi anza kwanza kutafuta kumtii Mungu kwa kumwamini Yesu Kristo kwa kuukubali wokovu na kumpatia maisha yako ayaendeshe.
Tengeneza mambo yako kwanza ndipo uyapate mema ya nchi. Unajua wapi ulipoanguka au nini kinachokuzuia usimuone Yesu anza kwanza kukiondoa na Yesu atakuandalia Fungu lako.
Usishindie maombi na kujiliza mbele za Mungu ukitaka mafanikio wakati unatambua moyoni mwako wapi umekosea na hujatengeneza bado, usikimbilie kumtwisha mzigo mchungaji wako kumuona hana upako kumbe wewe mwenyewe umebeba hatia na madhambi yanayokuzuia usisonge mbele, acha kubadili makanisa ukiamini utayapata mema anza kwanza kuubadili moyo wako ili hayo Mema yatakujia.
Sheria ni moja tu Anza kumtii Mungu kwanza ndipo upate mema yako na hakuna mema nje ya kumtii Mungu haijalishi umesoma sana, mzuri sana, una bidii sana, unajiweza kifedha au uwepo wa msaada mkubwa kwako.
Pasipo kumtii Mungu hata uoge kwenye p**a la mafuta ya upako utabaki kapuku vile vile mpendwa wewe, utazunguka makanisa yote na shida zitakuwa nawe.
HAKUNA MEMA PASIPO KUMJUA MUNGU.
Ayubu 22:21
[21]Mjue sana Mungu, ili uwe na amani;
Ndivyo mema yatakavyokujia.
HAKUNA MAFANIKIO PASIPO MUNGU.
Zaburi 127:1
[1]BWANA asipoijenga nyumba
Waijengao wafanya kazi bure.
BWANA asipoulinda mji
Yeye aulindaye akesha bure.
Usikeshe baharini usiku mzima k**a petro kwa bidii na ujuzi wako ila nenda kwa jina la Yesu pekee utafanikiwa na kupata zaidi.
Unaitaka familia bora, ndoa bora, mke bora, mume bora, maisha bora, afya njema, maisha marefu, mali na mafanikio kubali kumtii Yesu Kristo akupe yaliyo mema kwa ajili yako.
Pasipo kumtii Mungu tambua kuwa ulivyopaswa kuvitawala vitakutawala wewe na kukuendesha.
YESU ANAPIGA HODI KWAKO MFUNGULIE MLANGO KWANI ANASEMA.
Mathayo 11:28-30
[28]Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.
[29]Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;
[30]kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.
MWAMINI YESU KRISTO AKUTUE CHINI DHAMBI ZAKO ULE MEMA YA NCHI.
NIKUTAKIE WAKATI MWEMA.
Mwandishi ni: Msemaji Wa Injili
Mwenye whatsapp
WhatsApp Group Invite