29/01/2020
Mwendelezo wa Somo linaloitwa:
TAMBUA AINA YA KIBALI CHAKO ILI UPATE USTAWI KATIKA MAMBO YOTE!
Kuna aina kuu mbili za kibali ambazo ni:
1.) Kibali cha Asili katika Ufalme wa Mungu na kibali Cha Asili katika Ufalme wa giza,
2.) Kibali cha Siri katika Ufalme wa Mungu na kibali Siri katika Ufalme wa giza.
Aina ya kwanza ya Kibali nilishaifafanua katika sehemu zilipopita, na sasa tunaingia katika aina ya pili:
KIBALI CHA SIRI CHA KIUNGU
Kibali hiki hutolewa kwa mtu mmoja tu kwenye familia ambaye Mungu humfanya k**a ndiye mkombozi wa Familia ambapo mtu huyo huwa ni mwenye kubeba jukumu zito katika familia yake ama katika ukoo. Yeye hujiona kwamba ndiye mwenye hilo jukumu kutokana na kugundua kuwa bila yeye kuyapigania mambo yanayohusu familia yake, basi, hakuna mwingine anayeweza kuona tatizo k**a aonavyo yeye.
Kibali hiki cha Siri cha Kiungu hutambuliwa katika wakati wa jambo ambalo Mungu anataka kulitenda. Mfano mzuri tunauona kwa Rahabu kahaba! Alikuwa na kibali hicho cha kiungu na alifanikiwa kuiokoa nyumba yake!
Yoshua 2:1-24, 12, ''BASI SASA NAWASIHI NIAPIENI KWA BWANA KWA KUWA NIMEWATENDEA HISANI, YA KWAMBA NINYI NANYI MTAITENDEA HISANI NYUMBA YA BABA YANGU; TENA NIPENI ALAMA YA UAMINIFU YA KWAMBA MTAWAPONYA HAI BABA YANGU NA MAMA YANGU, NA NDUGU ZANGU WANAUME NA WANAWAKE, NA VITU VYOTE WALIVYO NAVYO, NA KUTUOKOA ROHO ZETU NA KUFA.''
Kwa wakati huu tunaona Rahabu alionekana ana Kibali cha Siri cha Kiungu ambacho kilisababisha wokovu wa nyumba yote ya baba yake. Kabla haya yote hayajatokea habari za Rahabu hazikujulikana kwa maana hakuonekana k**a anaweza kustahili kuiletea wokovu nyumba yake kwa sababu alikuwa na sifa ya ukahaba.
Kibali hiki cha Siri kinamhusu mtu maalum sana katika ukoo ambaye ndiye pekee huandaliwa kuleta wokovu kwa familia yake. Ni mtu asiyejulikana na watu kwamba kupitia yeye kipo kibali cha Mungu juu ya nduguze. Na mtu huyo ni mtu anayepata nafasi ya mara moja; na huitumia vizuri kuleta wokovu kwa nduguze. Huwa hana ishara yeyote ya wazi bali hutambuliwa na Mungu kwamba alikusudiwa ndani ya wakati, kuhakikisha usalama unapatikana wenye wokovu katika jamii ya watu fulani.
Waamuz 1:24-25, ''HAO WAPELELEZI WALIMWONA MTU ATOKA KATIKA HUO MJI, WAKAMWAMBIA, TAFADHALI,UTUONYESHE MAINGILIO YA MJI HUU, NASI TUTAKUTENDEA MEMA''
"BASI AKAWAONYESHA MAINGILIO YA MJI, NAO WAKAUPIGA MJI HUO KWA MAKALI YA UPANGA; LAKINI HUYO MTU WALIMWACHA AENDE ZAKE, NA WATU WOTE WA JAMAA YAKE.''
Mtu huyu bila shaka hakudhaniwa, ndio mana hata jina lake halijapewa nafasi ya kujulikana. Hicho ni kibali cha Siri cha Mungu kwa ajili ya kusudi la kuokoa jamii ya watu fulani watakaosababisha kusudi la Kiungu kutimia kupitia wao. Watu hao hufanyika sehemu ya kukamilika kwa mpango huo!
Kibali hiki kipo kwenye nafasi kubwa ya kupokea wageni!! Mathayo 25:35, ''KWA MAANA NALIKUWA NA NJAA MKANIPA CHAKULA; NALIKUWA NA KIU MKANINYWESHA; NALIKUWA MGENI MKANIKARIBISHA"
SIFA ZA MTU MWENYE KIBALI CHA SIRI.
- Ana wepesi wa kuelewa siri za Mungu, na
- Hugundua kwa urahisi nia ya waovu. Hali hiyo inamsaidia kumlinda yeye mwenyewe miongoni mwa watu wabaya bila yeye mwenyewe kugundua!
Ni vigumu mno mwenye kibali hiki kujigundua kabla ya Wokovu wa Mungu kumfikia. Yaani ni Siri ya Mungu mwenyewe kumtengenezea mazingira ya kulitumikia kusudi lake; hata pasipo yeye mwenyewe kuelewa kwamba ni mwenye kibali cha Siri. Hii ni kwa kuwa utendaji wa Kibali hiki hujulikana katika tukio maalum ambalo mwenye Kibali cha Siri hujikuta akipigania kusudi la Mungu litimie na waovu wasifanikiwe katika hila zao.
Mwenye Kibali hiki cha Siri anaweza hata kufanana na waovu kitabia katika jamii yake. Hali hii humpa nafasi ya kuishi kwa uhuru bila kudhaniwa kwamba kuna wakati hatokuwa upande wao.
Mungu ndiye mwenye kuruhusu hali hiyo kwa lengo la kumlinda mtu huyo asitofautishwe na wabaya mpaka wakati wa kusudi utimie kikamilifu.
Wakati mwingine Mungu humfanya mtu mwenye kibali cha siri kuwa na ushujaa katikati ya jamii yake. Hali hiyo inafunua Kibali cha Siri kwa sehemu ndogo sana ili kuwatia wivu maadui za Mungu; lakini Mungu hamtambulishi kwamba ndiye atakayewaletea wokovu mkuu nduguze.
Jamii hii ya mashujaa wenye Kibali cha Siri, Mungu huwafanya mashujaa hao wasieleweke katikati ya ndugu zao na hata jamii yao na mfano mzuri tunauona kupitia Yeftha katika kitabu cha Waamuzi 11:1-11:
Historia ya Yeftha inatueleza kwamba alikuwa ni mtoto wa mwanamke kahaba; akaishi na nduguze wa baba mmoja lakini baadae wakamfukuza kuwa hataweza kurithi pamoja nao; kwa sababu yeye ni mtoto wa mwanamke mwingine na wao wamezaliwa kwa mama mmoja.
Ndipo Yeftha akawakimbia nduguze; akakaa katikati ya jamii ya watu mabaradhuli akaungana nao. Majira yalipofika ya Kibali cha Siri kufunuliwa; nduguze wakashindwa vita na wazee wa mji wakamfuata ili aje vitani apate kuwashindia kwa maana alikuwa ni shujaa; na mapatano yao walimpa nafasi ya kuwa mtawala wao:
Waamuzi 11:5-6:
''WAKAMWAMBIA YEFTHA, NJOO WEWE UWE KICHWA CHETU ILI TUPATE KUPIGANA NA WANA WA AMONI. YEFTHA AKAWAAMBIA WAZEE WA GILEADI, JE NINYI HAMKUNICHUKIA MIMI NA KUNIFUKUZA NITOKE KATIKA NYUMBA YA BABA YANGU?
''BASI KWANI KUNIJILIA HIVI SASA WAKATI MLIO KATIKA TAABU?"
Hivi ndivyo Mungu alikuwa ameificha Siri hiyo ya Kibali ndani ya Yeftha; kupigania utawala wa nduguze ili wakae katika usalama; baada ya watesi wao kuangamizwa na mwenye Kibali akatambuliwa katika nafasi ya ukuu; ambapo mwanzo haikuonekana nafasi hiyo.
K**a isingekuwa ni Kibali cha Siri bila shaka Yeftha angeuawa na nduguze na ukombozi wa Taifa lake usingepatikana.
KUTAMBULISHWA KWA MWENYE KIBALI CHA SIRI
Mungu huruhusu mabaya yaonekane katika jamii ya mtu mwenye kibali cha siri ili atakapomtambulisha awe na kitu cha kufanya ili kuufunua ukombozi uliokuwa ndani yake.
Amina!
Kwa mawasiliano zaidi ikiwa unahitaji ufafanuzi wa suala lolote hapa kwenye somo unaweza kupiga simu namba +255 694 269331 au kutuma ujumbe kwa njia ya Messenger.
Mungu wa Mbinguni azidi kukubariki unapoendelea kutembelea ukurasa huu.