28/10/2025
SHUHUDA ZA MAOMBI YA KUVUNJA KUTA ZA YERIKO YALIYOFANYIKA KUANZIA TAREHE 08-15 OKTOBA 2025
USHUHUDA WA 5
Shalom mtumishi.
Namshukuru Mungu kwa wema wake na uaminifu wake katika maisha yangu. Mwaka huu umekuwa mwaka wa vita vikubwa sana kwangu, lakini katika yote hayo Mungu hajaniacha.
1. MUNGU AMERUDISHA HESHIMA YANGU
Kutosemeshwa kwa miaka mitano haikuwa jambo rahisi, hasa kwa watu ambao kiasili nilipaswa kuzungumza nao karibu kila siku. Ilikuwa kipindi cha upweke, maumivu, na maswali mengi moyoni.
Kulikuwa na watu waliokuwa wamenidharau, wakanisemea maneno ya uongo, wakanitukana, na wengine wakaniangalia k**a sifai chochote.
Lakini ninamshukuru Mungu wa rehema, kwa sababu hao hao waliokuwa wakinicheka na kunidharau, Mungu amewagusa na kubadilisha mioyo yao na sasa wameanza kuniambia tena, tena kwa heshima na utulivu mkubwa.
Kupitia hili nimejifunza kwamba Mungu pekee ndiye hurejesha heshima ya mtu.
Wakati wa Mungu ukifika, hakuna mtu, hali, wala nguvu yoyote inayoweza kuzuia kile alichokusudia kukifanya.
2. MUNGU AMEFUNUA SIRI KUPITIA MAOMBI
Wakati wa Maombi ya Yeriko, nilisukumwa rohoni kumuweka binti anayenisaidia kazi nyumbani katika agenda ya maombi, ingawa sikupanga kufanya hivyo.
Baada ya maombi, alijitahidi kutoroka, lakini majirani walimk**ata. Nilipopigiwa simu na kurudi nyumbani, nikagundua alikuwa amenibia pesa. Mungu alinifungua macho na kunilinda dhidi ya udanganyifu huo.
Kupitia tukio hili, nimejifunza jambo muhimu: tunapaswa kuwaombea wale wote tunaishi nao, kwa sababu maombi yetu yanaweza kuwasaidia, kuwakomesha waovu, na kufungua njia za wema ambazo hatuwezi kuzifanikisha wenyewe.
Hii ni ishara ya nguvu ya Mungu, yeye hufunua siri zilizofichika na hutoa ulinzi kwa wale wanaomtegemea.
3. MUNGU AMEANZA KUFUNGUA MILANGO YA UJENZI
Nilimlilia Mungu kuhusu suala la ujenzi wa nyumba yetu, nikaomba atufungulie milango na avunje vizuizi vyote vilivyokuwa vinatukwamisha.
Kwa kweli Mungu ni mwema! Kwa uweza wake, kazi imeanza kufanyika kwa kasi, na tunaendelea kuona maendeleo katika ujenzi wetu hatua kwa hatua.
4. MUNGU AMENIPA WEPESI NA UHURU WA KIROHO
Kwa muda mrefu nilitamani sana kunyoa nywele zangu, lakini haikuwa rahisi. Nilipomaliza maombi, nikaanza kukumbuka mambo ya zamani ambayo nilidhani ni ya kawaida, kumbe yalikuwa na mizizi ya kiroho.
Miaka miwili iliyopita nywele zangu mbili zilikatika, nikaunganishiwa. Baada ya muda nikaanza kukosa amani, nywele zikaanza kudumaa, kukosa nuru, na hatimaye kuharibika (zilioza kabisa). Nilihisi kutaka kunyoa lakini sikuwa na kibali; hata familia yangu hawakutaka nisifanye hivyo.
Nilianza kwa kupunguza nusu kwa nusu, kisha nikaendelea kusuka kwa kipindi cha miaka miwili, nilisuka mara moja tu kwa kila mwaka.
Wakati wa Maombi ya Malango mwezi Septemba 2025, hisia za kunyoa nywele zikaongezeka zaidi. Nilifumua nywele na kuendelea kutafakari, lakini nilipoanza Maombi ya Yeriko, nikasikia msukumo mkubwa rohoni wa kuzitoa kabisa.
Hatimaye niliamka na kutoa dreadlocks zote, na nilishangaa kuona wepesi usio wa kawaida na amani ya ajabu rohoni mwangu.
Kupitia hili, nimejifunza jambo kubwa sana kuhusu nywele, kwamba si kila kitu kinachoonekana cha kawaida ni cha kawaida. Mungu hutumia mambo madogo kutufundisha masomo makubwa ya kiroho.
Kwa kweli Mungu ni mwaminifu.
Ameonyesha upendo, ulinzi, na nguvu zake katika maisha yangu.
Utukufu, heshima, na sifa zote zimrudie Mungu wetu milele.