22/05/2026
Mada: “Je, Wanipenda?” – Wito wa Urejesho kwa Vijana wa Bukumbi
Katika Yohana 21:15-17, baada ya Ufufuko, Yesu anamkabili Petro kwa swali mara tatu: “Simoni, mwana wa Yohana, je, wanipenda?” Swali hili halikuwa la kumburuza Petro kwa sababu alimkana Yesu mara tatu usiku wa Mateso. Lilikuwa la kumponya, kumrejesha, na kumpa tena dhamana ya kuchunga kondoo.
1. Kuanguka ni sehemu ya safari, si mwisho wake
Petro alimkana Yesu kwa hofu. Sisi vijana wa Bukumbi pia tunamkana Kristo tunapomweka pembeni katika maisha yetu. Tunamkana tunapochagua starehe, marafiki, na mitandao badala ya sala na Sakramenti. Tunamkana tunapodanganya, kudharau wazazi, na kuingia katika uasherati na ulevi.
Mfano huu unafanana na nahodha wa Young African Sports Club ambaye hivi karibuni alijifunga goli la kujiumiza. Makosa hayo yamefanya mashabiki na baadhi ya wachezaji wenzake wamwone k**a msaliti. Moyoni mwake amekata tamaa, anaona ameshindwa na amewachanganya wote waliomwamini.
Kila kuanguka kunaleta aibu na hamu ya kujificha. Lakini k**a Petro, na k**a nahodha huyo, hatuachwi katika aibu yetu. Yesu anarudi na swali lile lile: “Je, wanipenda?”
2. Kanisa linawahitaji hata mkianguka
Yesu hakumwacha Petro kwa sababu ya udhaifu wake. Alimrudisha katika utume kwa kusema, “Chunga kondoo wangu.” Timu, kocha na viongozi wa Yanga bado wanamhitaji nahodha wao licha ya kosa lake. Hivyo ndivyo Kanisa linavyowahitaji ninyi vijana leo.
Kanisa halitafuti vijana wasiokosea kamwe. Linatafuti vijana wanaoamka kila waangukapo, wanaotubu dhambi zao, na wanaorudi katika utume. Ushuhuda wenu, sala yenu, na maisha yenu yanahitajika ili wenzenu wapate kuona uso wa Kristo.
Mkianguka, msikimbie. Kukimbia huongeza jeraha. Rudini kwa Yesu katika Sakramenti ya Toba. Rudini kwa moyo wa toba na kusema, “Bwana, wajua ya kuwa nakupenda.” Yeye husamehe, husahau, na hukurejesha kazini.
3. Urejesho unakuja kwa kutumwa tena
Baada ya kila “Ndiyo, nakupenda,” Yesu alimwambia Petro, “Chunga kondoo wangu.” Urejesho wa kweli haupatikani kwa kujificha, bali kwa kurudi kazini.
Nahodha wa Yanga anaweza kuwa nguzo ya ushindi ijayo ikiwa atakubali kurejeshewa na kurudi uwanjani kwa uaminifu. Hivyo ndivyo anavyowaita ninyi vijana wa Bukumbi. Lisheeni wenzenu kwa neno la kweli. Simameni kwa ajili ya ukweli shuleni, nyumbani, na mtaani. Onyesheni huruma ya Kristo kwa waliopotea. K**a Petro alirudi na kuwa mwamba wa Kanisa, ninyi pia mnaweza kurudi na kuwa nguzo ya Kanisa hapa Bukumbi.
Hitimisho
Vijana wangu, msikate tamaa kwa sababu ya udhaifu wenu. Kristo aliyemrejesha Petro ndiye yule yule leo. Anawatazama ninyi na kuuliza: “Je, wanipenda?”
Jibu lenu liwe si maneno tu, bali maisha yanayomwonyesha Kristo kwa wenzenu. K**a mlipomkana kwa matendo, rudi kwake kwa matendo ya uaminifu, unyenyekevu, na huduma.
“Bwana Yesu, wajua yote. Wajua ya kuwa nakupenda. Niponye, unirejeshe, unitume tena.”
Amina.