11/02/2023
Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Albert Chalamila alimpokea Askofu Dkt. Fredrick Shoo, Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, anayefanya ziara katika KKKT Dayosisi ya Kaskazini Magharibi, Bukoba.
Askofu Dkt. Shoo alianza ziara hiyo Februari 8, 2023na ameambatana na mwenyeji wake, Askofu Dkt. Abednego Keshomshahara wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini Magharibi. Katika mazungumzo yao Mhe. Chalamila alimweleza Askofu Dkt. Shoo juu ya mazingira mazuri ya uwekezaji, ikiwa ni pamoja na kupata mvua za uhakika misimu miwili kwa mwaka.
Mhe. Chalamila alimweleza Askofu Dkt. Shoo kwamba pamoja na Mkoa wa Kagera kuwa na wasomi wengi na mazingira mazuri ya uwekezaji, bado hali hiyo haijatafsirika vizuri katika vitendo ili kuweza kuinua uchumi wa Mkoa. Mhe. Chalamila alieleza kwamba ofisi ya Mkuu wa Mkoa inaendelea kushirikiana na wadau wengine kuhakikisha watu wengi zaidi wanawekeza na kuongeza uzalishaji katika nyanja mbalimbali ili kuinua kipato binafsi na uchumi wa jumla katika Mkoa.