29/11/2024
UTANGULIZI:
A) MADHUMUNI YA SOMO:
Madhumuni ya somo hili mpendwa mwana wa Mungu katika Kristo; kwanza kabisa ni kuimarisha nguvu ya kila mmoja aliyedhamiria kwa dhati ya moyo wake kuishi katika wokovu hata atakapoingia katika ule ufalme wa Baba. La pili ni kujenga uelewa juu ya huduma hii jinsi Mungu alivyoikusudia kuweka mwamko mioyoni mwetu. Na la tatu ni kukufanya msomaji uone jinsi ilivyo muhimu kuweka Neno la Mungu ndani yako ili kupata jawabu la maisha yako ya kiroho na kimwili.
B) NENO NI NINI?
Tunaanza na NENO; hii inamaanisha ujumbe wa aidha matamshi ya kitu chochote au maandishi. Ninasema matamshi ya kitu chochote kwasababu Biblia yangu inaniambia hata punda amesema neno. Biblia inasema hivi; ❝Bwana akakifunua kinywa cha yule punda, naye akamwambia Balaamu, Nimekutenda nini, hata ukanipiga mara tatu hizi?❞
—Hesabu 22: 28 (Biblia Takatifu)
Punda alisema NENO.
Lakini mara nyingi tumezoea ujumbe unao eleweka ni kutoka kwa mwanadamu; kumbe hata viumbe katika ulimwengu huu na ule wa roho pamoja na Mungu mwenyewe wanatupatia jumbe mbalimbali.
Twende kwenye lengo!
NENO katika Biblia; ni ujumbe wa Mungu maalum kwaajili yetu; Neno ni Mungu. Neno ni Yesu Kristo mwenyewe, aliye mwokozi wa maisha yetu.