31/05/2026
MASOMO YA MISA, JUMATATU YA JUMA LA TISA, KIPINDI CHA KAWAIDA, MWAKA II, KUMBUKUMBU YA MT. YUSTINO, SHAHIDI, JUNI 1, 2026
RANGI YA KILITURJIA: NYEKUNDU ❤
SOMO LA KWANZA
2 Petro 1:2—7
Ametuahidia ahadi nzuri na kuu, ili kwa njia ya ahadi hizi muweze kushiriki umungu wake.
Somo katika barua ya pili ya Mtakatifu Petro
Ndugu: Neema iwe nanyi, na amani tele katika kumjua Mungu na Yesu, Bwana wetu. Kwa uwezo wake wa kimungu ametujalia tunayoyahitaji kwa uzima na ibada ya kweli akituwezesha kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe. Hivyo ametujalia ahadi kubwa ajabu, kusudi kwa hizo mpate kuishiriki tabia ya kimungu, na kuepuka maangamizi yaliyopo duniani kwa sababu ya tamaa mbaya, Kwa hiyo, fanyeni kila bidii kuunganisha imani yenu na fadhila, tena fadhila na ujuzi, ujuzi na kiasi, kiasi na udumifu, udumifu na uchaji wa Mungu, uchaji wa Mungu na undugu, tena undugu na upendo.
NENO LA BWANA... TUMSHUKURU MUNGU
ZABURI YA KUITIKIZANA
Zaburi 91:1—2, 14—15ab, 15e—16 (K. 2b)
K. Ee Mungu wangu, ninakutumaini.
Akaaye katika ulinzi wake Aliye Juu,
atapumzika katika kivuli cha Mwenyezi.
Nitamwambia Bwana, "Wewe kimbilio langu na ngome yangu,
Mungu wangu, ninayemtumaini!" K.
Kwa kuwa ameambatana nami katika upendo, nitamwokoa,
nitamlinda, kwa kuwa analijua jina langu.
Aniitapo, nitamwitikia; nitakuwa pamoja naye katika taabu. K.
Nitamwokoa na kumpa utukufu.
Kwa wingi wa siku, nitamridhisha;
nami nitamwonyesha nguvu ya wokovu wangu. K.
SHANGILIO LA INJILI
TAZAMA UFUNUO 1:5ab
K. Aleluya. W. Aleluya.
K. Yesu Kristo, wewe ni shahidi mwaminifu, mzaliwa wa kwanza wa wafu; umetupenda, na umezisafisha dhambi zetu kwa damu yako.
W. Aleluya.
SOMO LA INJILI
MARKO 12:1—12
Walimchukua yule mwana mpendwa, wakamwua, na wakamntupa nje ya shamba la mizabibu.
† Somo la Injili takatifu ilivyoandikwa na Marko
Wakati ule: Yesu alianza kusema kwa mifano na makuhani wakuu na waandishi na wazee]. Mtu alipanda shamba la mizabibu, akalizungushia wigo, akachimba shimo la kukamulia zabibu, akajenga kilindo, akawapangisha wakulima, akaenda ugenini. Wakati wake alimtuma mtumishi aende kwa wale wakulima kupokea kwao matunda ya mizabibu. Nao wakamk**ata, wakampiga, wakamrudisha mikono mitupu. Akamtuma mtumishi mwingine aende kwao. Naye wakampiga kichwani, wakamtukana vibaya. Akamtuma mwingine, naye wakamwua. Na vivyo hivyo tena wengi; wengine wao waliwapiga, na wengine waliwaua. Alibaki bado mmoja, ndiye mwana wake mpendwa. Mwisho alimtuma huyo aende kwao akisema, "Watamjali mwanangu." Lakini wale wakulima wakasemezana, Huyu ni mrithi. Haya tumwue, na urithi utakuwa wetu.' Basi wakamk**ata, wakamwua, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu. Basi, bwana wa shamba la mizabibu atafanya nini? Atakuja na kuwaangamiza wale wakulima, na shamba la mizabibu atawapa wengine. Hamjasoma bado andiko hili: Jiwe walilolikataa waashi limekuwa kiungo cha pembeni; hayo yametendwa na Bwana, nayo ni mwujiza machoni mwetu?" Nao walitamani kumk**ata, kwa maana walitambua ya kwamba aliwalenga wao wenyewe kwa mfano huo. Lakini waliuogopa umati wa watu. Basi, wakamwacha, wakaenda zao.
INJILI YA BWANA... SIFA KWAKO EE KRISTO