08/05/2026
UKIANZA KUISHI K**A MUNGU ANAVYOTAKA UTAANZA KUWASHANGAZA WATU WANAOKUJUA
Mt 13:54-55 SUV
[54] Na alipofika nchi yake, akawafundisha katika sinagogi lao, hata wakashangaa, wakasema, Huyu amepata wapi hekima hii na miujiza hii? [55] Huyu si mwana wa seremala? Mamaye si yeye aitwaye Mariamu? Na nduguze si Yakobo, na Yusufu, na Simoni, na Yuda?
Badiliko la mtu la ndani linaanza pale anapomwamini Yesu Kristo, pale anapoanza kuliishi neno la Mungu, anaanza kuwa mtu wa tofauti kwenye ulimwengu huu.
Kuna maeneo watu walimjua mtu alivyo, wengine alikua nao, wengine alisoma nao, wengine ni ndugu zake, anapoanza kutembea katika kusudi la Mungu anakuwa mtu tofauti kabisa na wa kushangaza watu.
Utakuwa shahidi wa hili, kuna watu uliwazoea kwa namna fulani kutokana na vile unawafahamu siku nyingi, ila baadaye wanakuwa watu wenye utofauti mkubwa na kujitenga kabisa na maisha fulani.
Utofauti wa mtu unaletwa na Mungu mwenyewe, anapoanza kutembea na kuongozwa na Mungu katika maisha yake, anakuwa mtu wa tofauti kabisa.
Huwezi ukawa umeokoka, umejazwa na Roho Mtakatifu, umejaa neno, na maombi, ukawa mtu yule yule.
Utaanza kuleta sintofahamu kwa watu wako wa karibu, watu wanaokujua wewe ni mtoto wa fulani, utofauti huo unakuja baada ya Mungu kukubadilisha.
Tegemea kukutana na badiliko la kweli katika maisha yako baada ya kumpokea Yesu Kristo, baada ya kujazwa Roho Mtakatifu, na baada ya kujaa neno la Mungu.
Hutabaki k**a ulivyo, na unajiona upo k**a ulivyo, yaani huoni tofauti kabla ya kuokoka na baada ya kuokoka, basi jitafakari upya uone kipi kimepungua kwako.
Soma neno ukue kiroho
Liwe jua iwe mvua soma biblia na kutafakari
Mungu akubariki sana