Chapeo Ya Wokovu

Chapeo Ya Wokovu Karibu mafundisho ya NENO la Mungu ukue KIROHO. Jiunge na channel yetu ya WhatsApp=>>https://whatsapp.com/channel/0029VbCp7ho4SpkEtKlTHK2I

11/08/2026

HUKUCHAGULIWA KWA BAHATI MBAYA UKAE KWENYE NAFASI ULIYONAYO LEO

Mdo 6:3-4 SUV
[3] Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; [4] na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno.

Napenda niongee na wale ambao wamechaguliwa katika nafasi mbalimbali katika kundi la Mungu, au kanisa la Mungu, au kusanyiko la ki-Mungu.

Tunaweza kufikiri nafasi tuliyopewa ni nafasi k**a zingine za kawaida, tunaweza kuchukulia kwa uzito mdogo zile nafasi tulizopewa au kuchaguliwa.

Hatujui au hatujiulizi kuwa kuchaguliwa kwetu ilitokea nini mpaka watumishi wa Mungu wakaa na kuona vyema fulani na fulani wakae katika nafasi fulani.

Hupaswi kujichukulia kawaida na kujiona mnyonge, waliokuweka hapo hawakulala Leo na kuamka kesho yake wakakuweka. Ulikuwepo mchakato mrefu wa kukupata wewe.

Lipo jukumu kubwa ambalo waliokuweka waliona unaweza kulifanya na wao wakafanya majukumu mengine ya ki-Mungu.

Mdo 6:2 SUV
[2] Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani.

Unamwona mchungaji, Askofu, au yeyote yule aliyekaa kwenye nafasi fulani kuliongoza kundi la BWANA kuona vyema kukuchagua wewe au mtu fulani akae kwenye nafasi fulani, kwa akili ya kawaida utaona ni matakwa yake, bila kujua MUNGU amesema nini naye.

Sio hivyo tu, kwenye huduma/madhehebu mbalimbali wameweka miongozo ya idara, watu huchaguliwa kila baada ya kipindi fulani, wengine huchaguliwa kuwa shemasi, wazee wa kanisa, katibu na waratibu wa idara mbalimbali kanisani.

Kufanya hivyo ni kurahisisha utendaji wa Ki- Mungu kanisani, usipoelewa utatumika kwa mazoea na kwa viwango vya chini, bila kufanya unajikosesha baraka za Mungu zinazotaka na nafasi uliyowekwa.

Wakati mwingine Mungu hutupa kibali cha kukaa kwenye nafasi za chini kabisa, tukiwa waaminifu hutuweka nafasi zingine za juu zaidi.

Leo unaweza kujiona upo kwenye nafasi fulani ndogo kabisa kwenye hiyo huduma ya Mungu au kanisa, ukajua ni jambo la kawaida au watu hawajui heshima yako huko kazini kwako au kwenye jamii. Ama kwenye mipango yako unayo maono makubwa, ukaona nafasi uliyopewa hailingani na viwango vya maono yako, ukaidharau, bila kujua ulikuwa msingi wako wa majaribio wa kukupeleka kwenye eneo Mungu anataka ufike.

Napenda kukuasa jambo hili, ikiwa umechaguliwa na kuwekewa mikono utumike kwenye nafasi fulani, usije ukaipuuza na kuifanya kwa viwango vya chini. Watu waliomba na kukuona unafaa, unachokifanya kwa uzembe halikuwa kusudi la Mungu, upo nje ya mapenzi ya Mungu.

Soma neno ukue kiroho
Liwe jua iwe mvua soma biblia na kutafakari
Mungu akubariki sana
Samson Ernest

05/08/2026

‼️Usipuuze hatua ndogo ndogo katika maisha yako, ukiangalia biblia ni kubwa sana, ukisikiliza watu wanavyoiongelea unaweza usiisome ukaimaliza, ila ukiamua kujiwekea utaratibu wa kusoma sura moja kila siku na kupata muda wa kutafakari, baada ya muda utaimaliza. Sifa sio kumaliza na kutulia, unamaliza na kuanza tena, unakuwa utaratibu wa maisha yako yote.

‼️Shalom, baada ya safari ya kusoma kitabu cha Yohana, leo tunahitimisha safari hii, na kesho tunaanza safari mpya ya ku...
04/08/2026

‼️Shalom, baada ya safari ya kusoma kitabu cha Yohana, leo tunahitimisha safari hii, na kesho tunaanza safari mpya ya kusoma kitabu cha matendo ya mitume.
Hongera sana kwa kusoma kitabu cha Yohana siku zote 21 bila kuacha hata siku moja.
Mungu akubariki sana

28/07/2026

USIVUNJE UHUSIANO WAKO NA MUNGU

Yn 15:14 SUV
[14] Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo.

Mtu yeyote kuwa na urafiki na mtu mwingine, lazima kuna maeneo waliona wanaendana.

Urafiki wetu au ushirika wetu na watu wengine hautoki hewani, unatokana na mahusiano yetu yaliyounganishwa na jambo fulani linaloendana.

Waamini tunakuwa jamii moja na familia moja kwa sababu tumeunganishwa na Kristo.

Kile kitu kilichotuunganisha kinapopotea, ule urafiki hufifia kisha kupotea kabisa.

Urafiki wetu na Yesu unakuja pale tunapomwamini na kuliishi neno lake, hapo tunakuwa na uhusiano mzuri sana naye.

Tunapotoka nje na hapo, urafiki wetu na Yesu huisha hapohapo, na hapo tunakuwa tumekaribisha marafiki wengine.

Kuharibu uhusiano wetu na Yesu ni jambo hatari sana kwa maisha ya mwamini, anaweza kuharibu maisha yake kwa kuanzisha urafiki na adui shetani.

Tunaweza kulinda uhusiano wetu na Yesu kwa gharama yeyote ile, tuhakikishe tupo vizuri na Yesu.

Soma neno ukue kiroho
Liwe jua iwe mvua soma biblia na kutafakari
Mungu akubariki sana

27/07/2026

UKIKIPENDA KITU UTAPAMBANA UKIPATE NA KIBAKI KATIKA MIKONO YAKO

Yn 14:23 SUV
[23] Yesu akajibu, akamwambia, Mtu akinipenda, atalishika neno langu; na Baba yangu atampenda; nasi tutakuja kwake, na kufanya makao kwake.

Kila mmoja mpaka kufika umri alionao sasa, amewahi kupenda kitu katika maisha yake, hata k**a kwa wengine kinaonekana ni kitu cha kawaida.

Baada ya kukipenda hicho kitu mtu huyu atahakikisha anachukua hatua kuhakikisha anakipata hicho kitu.

K**a mtu alikuwa na kitu alihakikisha kinaendelea kubaki kwenye mikono yake.

Ukiona mtu anakuambia ameshindwa kupata kitu fulani, huenda sababu ikawa hajakipenda vizuri hicho kitu.

Upendo una nguvu zaidi vile tunaweza kuufafanua hapa, mtu akipenda kitu huwezi kumzuia zaidi utamchelewesha kukiendea na kukikapata hicho kitu, mazuio ambayo yanaweza yasiwe na matunda yeyote.

Mtu akimpenda Yesu na akamwelewa vizuri juu ya utendaji wake katika maisha yake, anaweza kufanya chochote kwa ajili ya Yesu.

Ukiona mtu unamtoa kirahisi kwa Yesu ujue huyo Upendo wake ulikuwa nusu nusu, yeyote aliyekaa sawasawa na Yesu hawezi kuondolewa kiurahisi moyoni mwake.

Yn 14:24 SUV
[24] Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka.

Huwezi kusema sina muda wa kusoma biblia, ujue huna Upendo ndani yako, mwenye upendo na Mungu wake atakuwa naye karibu kwa njia ya kusoma biblia na kutafakari.

Huwezi kusema mimi nimekuwa mtu mzima sasa siwezi kuendelea na mambo ya Yesu, huko ni kupotea na kukosa mambo aliyonayo Yesu katika maisha yako.

Upendo wetu uwe juu zaidi mbele za Mungu, hatutokuwa na visingizio vingi tulivyonavyo leo vya kutuzuia kulitimiza lile kusudi la Mungu.

Ukiona unakuwa na visingizio vingi juu ya jambo fulani ujue hujakipenda, mtu akipenda kitu atapambana mpaka akipate hicho kitu.

Soma neno ukue kiroho
Liwe jua iwe mvua soma biblia na kutafakari
Mungu akubariki sana

22/07/2026

USIJITOE KWENYE USALAMA WAKO

Yn 10:28-29 SUV
[28] Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. [29] Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu.

Ukisikia mtu yupo mikono salama bila shaka unapata picha ya uhakika mtu huyo analindwa na yupo kwenye ulinzi wa uhakika, na hakuna kitakachomdhuru katika maisha yake.

Mtu akikuambia mtoto wako yupo mikono salama, k**a ulikuwa na wasiwasi juu ya jambo fulani unapata utulivu wa ndani na kukaa vizuri.

Walio ndani ya Yesu wapo salama, adui hawezi kuwafanya chochote, haya sio maneno matupu au ya hewani, huu ni ukweli ulio wazi kabisa.

Unaweza kujiuliza inakuwaje mtu anasema ameokoka au yupo ndani ya Yesu na anasumbuliwa na Shetani?

Huyu mtu anaweza akawa hana neno la Mungu, anakuwa amejaa hofu, wasiwasi au mashaka mengi, anateswa hayo na hayo. Na wakati mwingine Mungu huruhusu amtese kwa mapenzi yake mwenyewe.

Wengine wanasema wapo ndani ya Yesu, au wanasema wameokoka, au wanafanya na huduma kabisa, ila kwa upande mwingine wanafanya mambo yanayomchukiza Mungu, na kumfurahisha Shetani.

Roho Mtakatifu hakai kwenye mchanganyo alionao mwamini, anapokaa pembeni Shetani anapata nafasi ya kutosha kumtumikisha huyo mtu anavyotaka.

Adui Shetani amekuja mara nyingi kwenye maisha ya wana wa Mungu, ila hakuweza kuwadhuru kutokana na ulinzi walionao kutoka kwa Baba yao wa mbinguni.

Nkuhakikishie unao usalama wa kutosha ndani ya Yesu Kristo, unaweza kupinga kutokana mafundisho uliyonayo ila ukweli hutobadilishwa na mtazamo ulionao juu ya Yesu.

Usijitoe kwenye mikono salama ya Yesu, upo salama, na unayo ahadi ya uzima wa milele baada ya maisha haya hapa duniani.

Soma neno ukue kiroho
Liwe jua iwe mvua soma biblia na kutafakari
Mungu akubariki sana
Samson Ernest

21/07/2026

KUTOKUJUA MENGI KUHUSU YESU HAKUKUZUII KUSHUHUDIA KILE AMEKUTENDEA KWAKO

Yn 9:25 SUV
[25] Basi yule mtu akajibu, Kwamba yeye ni mwenye dhambi sijui. Najua neno moja, kuwa mimi nalikuwa kipofu na sasa naona.

Inawezekana kwamba huna mambo mengi sana unayoyajua kuhusu Yesu Kristo, ila kuna kitu kikubwa ametenda kwako.

Tunaona hili kwa kipofu aliyeponywa macho yake, alichokuwa anakijua alikuwa haoni sasa anaona.

Hakujua sana mengi kumhusu Yesu, alichokuwa anakijua ni kimoja tu, alikuwa haoni, ila alipokutana na Yesu akamponya macho yake.

Kubwa ni hilo, hujui neno sana ila unajua Mungu anatenda makuu katika maisha yetu, kwa sababu kuna eneo umekutana naye uso kwa uso akibadilisha maisha yako.

Ukitendewa jambo kubwa huwezi kukosa cha kusema mbele za wale wanaomkataa Yesu, utakuwa na usemi mwepesi ila uliobeba ujumbe mzito.

Kitendo cha kusema hivi;
Yn 9:25 SUV
[25] Basi yule mtu akajibu, Kwamba yeye ni mwenye dhambi sijui. Najua neno moja, kuwa mimi nalikuwa kipofu na sasa naona.

Hii ni kauli ya mtu aliyekutana na Yesu kweli kweli, akaondoa kabisa ile shida iliyomsumbua miaka mingi, au tangu kuzaliwa kwake ana shida hiyo.

Si kila mtu anaweza akawa na ushuhuda unaomfanya apuuze kelele zote za kumpinga Yesu na kumkataa katika maisha yao.

Siku mtu akikutana na uponyaji wa Yesu k**a wa kipofu, hatakuwa na maneno mengi, maneno yake yatakuwa k**a hivi; sijui mnasema Yesu sio Mungu ila ninachojua niliombewa kwa jina la Yesu nikapona.

Maneno ya kupinga na kumkataa Yesu huisha pale mtu anapokutana na Yesu sawasawa, acha maisha ya jumla, ila mtu aliyekutana na Yesu kibinafsi hawezi kuwa na maneno mengi.

Yesu anatenda hata sasa, aliye tayari kubadilishwa na BWANA atabadilishwa kwa uhakika, aliye tayari kufanywa upya na akawa mtu mpya mwenye tabia njema Inawezekana.

Soma neno ukue kiroho
Liwe jua iwe mvua soma biblia na kutafakari
Mungu akubariki sana
Samson Ernest

20/07/2026

WANAOSEMA UONGO WANAAMINIKA NA WANAOSEMA UKWELI HAWAAMINIKI

Yn 8:45 SUV
[45] Nami, kwa sababu nasema iliyo kweli, hamnisadiki.

Yesu alikuwa anasema ukweli, ila kuna watu walikuwa hawamwelewi kabisa, wao walikuwa na mambo yao wanayoyaamini.

Utakuwa shahidi wa hili, mara nyingi watu huwa wanakimbilia kwenye uongo kuliko ukweli, kwa sababu unavutia na kuwafariji kwenye mambo yao maovu.

Mtu akitokea anadanganya na kuwafariji watu kwenye eneo wanalolipenda, atakuwa na watu wengi sana wanaompenda na kumfuata.

Uongo wakati mwingine unavutia sana kuliko ukweli, ndio maana unapendwa na wengi.

Yn 8:46 SUV
[46] Ni nani miongoni mwenu anishuhudiaye ya kuwa nina dhambi? Nami nikisema kweli, mbona ninyi hamnisadiki?

Watu wanaweza wasikuamini kabisa, si kwa sababu unasema uongo, ni kwa sababu unasema ukweli.

Si kila mtu anayeaminiwa ni mkweli, na si kila mtu asiyeaminiwa ni muongo, watu wanaweza wasikuamini kabisa kutokana na ukweli unaousema.

Haipaswi kukupa shida wewe unayesema ukweli alafu watu hawakuelewi unachosema au kuwaambia, na isikutishe unapokuwa na maadui kutokana na kusimamia ukweli.

Isikupe kuvimba kichwa kwa sababu watu wanakusikiliza na kukufuata, huku unajua unachowaambia watu ni uongo, na yote unayoyafanya ni ya uongo.

Soma neno ukue kiroho
Liwe jua iwe mvua soma biblia na kutafakari
Mungu akubariki sana

18/07/2026

Soma neno ukue kiroho

16/07/2026

USIRUDIE DHAMBI LISIJE LIKAKUPATA JAMBO BAYA ZAIDI

Yn 5:14 SUV
[14] Baada ya hayo Yesu akamkuta ndani ya hekalu, akamwambia, Angalia, umekuwa mzima; usitende dhambi tena, lisije likakupata jambo lililo baya zaidi.

Matatizo mengine tunayafungulia mlango wenyewe, mlango ambao unaingiza kila tatizo la kutuumiza kiroho na kimwili.

Tunaweza kufikiri magonjwa tunayougua ni magonjwa ya kawaida k**a mengine, ila mengine yanatokana na kujitenga na Mungu kwa matendo yetu maovu.

Jambo hili sio geni kwetu, tumeona watu wakipimwa na kukosekana ugonjwa wanaoumwa, au mtu anajulikana shida yake ila akipewa dawa za kutibu hilo tatizo haliponi, hata k**a atabadilisha kila dawa.

Matatizo mengine hayapo kimwili tu, yapo mpaka kiroho, unaweza kuhangaika kutibu kimwili hilo tatizo likashindikana kupona.

Tunajifunza kwa mgonjwa huyu aliyeponywa na Yesu, alipewa tahadhari ya kutorudia kufanya dhambi tena.

Ikiwa angerudia kufanya dhambi, lingempata Jambo baya zaidi ya Mwanzo, hili suala halikupaswa kuchukuliwa kawaida, lilipaswa kuchukuliwa kwa uzito mkubwa k**a ilivyo leo hatupaswi kulipuuza.

Tunaweza kukimbilia uponyaji wa ki-Mungu, hili tunalifanya tulio wengi, tunakimbilia miujiza ya uponyaji kuliko kuwa na uhusiano mzuri na Mungu, tukishaponywa tunarudi kwenye maisha yetu ya dhambi.

Mara nyingi hali zetu huwa mbaya zaidi ya Mwanzo, huwa tunaanza kufikiri hatukupata msaada wa Yesu, kumbe baada ya kupata uponyaji tulirudia maisha yetu ya dhambi.

K**a nilivyoanza kusema, si kila ugonjwa ni wa kawaida, magonjwa mengine yanaonekana ni ya kawaida lakini huwezi kuyatibu na dawa za hospital, isipokuwa yatapona kwa Jina la Yesu tu.

Yupo atazunguka kwa waganga wote wa kienyeji, huo ugonjwa hutokaa upone kwa sababu ya matendo yake maovu, na kwenda kwa huko ni kudhidi kujichafua zaidi.

Ukiombewa ukapona, iwe ni mapepo au ugonjwa wowote ule hakikisha hurudii maisha ya dhambi, hiyo ndio itakuwa salama yako.

Sio hivyo tu, tuepuka maisha ya dhambi, kwa sababu ni mlango wa magonjwa/matatizo mengi katika maisha yetu.

Soma neno ukue kiroho
Liwe jua iwe mvua soma biblia na kutafakari
Mungu akubariki sana

Address

Pembe
Singida

Opening Hours

Monday 09:00 - 18:00
Tuesday 09:00 - 18:00
Wednesday 09:00 - 18:00
Thursday 09:00 - 18:00
Friday 09:00 - 18:00
Saturday 09:00 - 18:00
Sunday 00:30 - 18:00

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Chapeo Ya Wokovu posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Place Of Worship

Send a message to Chapeo Ya Wokovu:

Shortcuts

Share