22/08/2026
MUNGU NI MKUU KULIKO TATIZO UNALOLIONA
KUTOKA 15:3–7
"“BWANA ni mtu wa vita, BWANA ndilo jina lake. Magari ya Farao na jeshi lake amewatupa baharini; maofisa wake wateule wamezama katika Bahari ya Shamu. Vilindi vimewafunikiza; walizama vilindini k**a jiwe.
BWANA, mkono wako wa kuume umepata fahari kwa uwezo; BWANA, mkono wako wa kuume wawasetaseta adui. Kwa wingi wa ukuu wako wawaangusha wanaokupinga; waituma hasira yako, nayo huwateketeza k**a mabua makavu.”
TAFAKARI
Mungu ni mkuu kuliko jambo lolote tunaloliwaza au kuliona. Wana wa Israeli walitambua ukuu wake baada ya kuvuka Bahari ya Shamu na kuliona jeshi la Farao likizama baharini.
Ingawa walikuwa wameshuhudia mapigo kumi yaliyompata Farao na jinsi Mungu alivyowatoa Misri, walipoona jeshi la Farao likiwakaribia, walijawa na hofu kana kwamba Mungu hakuwahi kuwaokoa. Walisahau kwamba Mungu aliyewatoa Misri ndiye aliyekuwa pamoja nao mbele ya Bahari ya Shamu.
Nasi wakati mwingine hutazama ukubwa wa tatizo na kusahau ukuu wa Mungu. Tunauona mlima ulio mbele yetu lakini tunasahau njia ndefu ambazo tayari Mungu ametuvusha. Hakuna mlima unaofika angani, wala hakuna bahari iliyo kubwa kuliko Muumba wake.
Mungu wetu ni mkuu kuliko vyote vilivyo duniani na mbinguni. Kabla hajaviumba, “nchi ilikuwa ukiwa, tena utupu, na giza lilikuwa juu ya uso wa vilindi.” Lakini Mungu alisema nuru iwepo, nayo ikawa. Hata giza linapoingia katika maisha yetu, Mungu anaweza kuliamuru na kulitoa nuru.
✍🏼Changamoto ni sehemu ya safari ya maisha. Usitazame tu mlima ulio mbele yako; kumbuka pia mabonde, dhoruba na njia ngumu ambazo tayari umezipita. Mungu aliyekuvusha wakati ule hajabadilika. Bado yupo pamoja nawe; hasinzii wala halali usingizi.
✍🏼Mungu ni mkuu kuliko njia unayopita, tatizo linalokusumbua na hofu inayotaka kuutawala moyo wako. Usipime uwezo wa Mungu kwa ukubwa wa tatizo lako; pima tatizo lako kwa ukuu wa Mungu wako.
✍🏼Kwa kuwa umeamka salama na umejaliwa uhai, mtie moyo aliyevunjika moyo, mwombee anayepitia njia ngumu, mshike mkono aliyeanguka, msaidie mwenye uhitaji na mpe tumaini aliyekata tamaa. Huenda unayolalamikia ni mambo ambayo mwingine anamwomba Mungu ayapate.
MUHIMU KUFAHAMU.,Usitazame ukubwa wa tatizo lako; mtazame Mungu aliye mkuu kuliko tatizo hilo. Mungu aliyekuvusha jana bado anaweza kukuvusha leo.