06/09/2026
SOMO: KUBATIZWA KIBIBLIA NA KUITIMIZA HAKI YOTE
UFUFUO NA UZIMA MOROGORO
BY BISHOP PROF. GODSON ISSA ZACHARIA
JUMAPILI SEPTEMBA 6, 2026
Neno ubatizo linatokana na neno la kiyunani “Baptiso” lenye maana ya “kuzamisha”. Hivyo basi ili mtu abatizwe lazima azamishwe kwenye maji, huu ndio ubatizo wa Kibiblia. Yesu mwenyewe ambaye ndiye Bwana na mwokozi wa maisha yetu alibatizwa kwa kuzamishwa kwenye maji na Yohana mbatizaji.
Kumekuwa na mafundisho mengi potofu kuhusu ubatizo lakini ukweli ni kwamba ubatizo wa Kibiblia unafanyika kwenye maji mengi ambapo mtu huzamishwa. Watoto wadogo hawawezi kubatizwa kwa sababu hawana uelewa wa neno la Mungu, watoto wadogo wanabarikiwa au kuwekwa wakfu.
Ubatizo wa Biblia
“Wakati huo Yesu akaja kutoka Galilaya mpaka Yordani kwa Yohana ili abatizwe.
Lakini Yohana alitaka kumzuia, akisema, Mimi nahitaji kubatizwa na wewe, nawe waja kwangu? Yesu akajibu akamwambia, Kubali hivi sasa; kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote. Basi akamkubali”.(Mathayo 3:13-15)
Bwana Yesu alikwenda mto Yordani kwenye maji mengi ambapo Yohana alikuwa anawabatiza watu. Yohana alitaka kumzuia lakini Yesu alimwambia anataka abatizwe ili aitimize haki yote. K**a Yesu ambaye ni mwana wa Mungu alikubali kubatizwa ubatizo wa maji mengi ili aitimize haki yote, mimi na wewe ni nani hata tupinge ubatizo wa maji mengi?
Wapo watu wanasema k**a mnataka kubatizwa k**a Yesu na nyie muende Yordani. Huu ni upotoshaji na ukosefu wa maarifa. Ubatizo wa Kibiblia ili utimie si lazima kwenda mto Yordani bali lazima maji mengi yawepo ya kumfanya mtu kuzama.
Hatua za Ubatizo wa Biblia
(i)Kuamini
Kabla ya mtu hajabatizwa anatakiwa kuamini; sio kumuamini mke/mume wake, mjomba, shangazi, bibi, babu, mchungaji, paroko, askofu, nabii, mtume bali aliamini neno la Mungu. Kuna watu walibatizwa walipokuwa watoto wadogo halafu wakaamini baadaye walipokuwa wakubwa jambo ambalo si sahihi. Unatakiwa uamini kwanza halafu ubatizo ufuate kwa sababu huwezi kuvaa suti kabla hujavaa nepi.
“Basi imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo”(Warumi 10:17)
Krispo alikuwa kiongozi mkubwa wa Kanisa lakini jambo la ajabu alikuwa bado hajamuamini Yesu. Baada ya kulisikia neno la Mungu aliamini, alitubu na akabatizwa.
“Na Krispo, mkuu wa sinagogi, akamwamini Bwana pamoja na nyumba yake yote. Wakorintho wengi waliposikia, waliamini, wakabatizwa".(Matendo 18:8)
(ii)Lazima kuwe na maji tele
“Yohana naye alikuwa akibatiza huko Ainoni, karibu na Salimu, kwa sababu huko kulikuwa na maji tele; na watu wakamwendea, wakabatizwa”.(Yohana 3:23)
Yohana alikwenda kubatiza Ainoni kwa sababu kulikuwa na maji tele. K**a Yohana ambaye ndiye mbatizaji mkuu alikuwa anawabatiza watu kwenye maji mengi tunatakiwa kujiuliza huu ubatizo wa kumpaka mtu maji kichwani umetoka wapi?
“Filipo akafunua kinywa chake, naye, akianza kwa andiko lilo hilo, akamhubiri habari njema za Yesu. Wakawa wakiendelea njiani, wakafika mahali penye maji; yule towashi akasema, Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe”?(Matendo 8:26-35-36)
Towashi alipoyaona maji mengi alimuomba Filipo ambatize kwa sababu alijua ili ubatizwe kwa usahihi sharti maji mengi yawepo. K**a ulibatizwa kwenye kikombe leo ufahamu ukweli huu na ubatizwe Kibiblia.
(iii)Kutubu dhambi
Kutubu dhambi maana yake ni kuacha uasi, kuacha matendo mabaya na kumuamini Mungu.Baada ya kuamini unatakiwa kutubu dhambi zako halafu ubatizo ufuate.Mtu anayetubu dhambi zake huwa anapata leseni ya kubatizwa. Yesu anasema makahaba na watoza ushuru watawatangulia kuingia mbinguni kwa sababu mtu yeyote anayetubu Mungu humsamehe.
Shetani hapendi kuona mtu anatubu ili aendelee kummiliki ndiyo maana unaweza kumuona kiongozi mkubwa wa serikali amelitia taifa hasara kubwa lakini hawezi kujitokeza hadharani na kuomba radhi. Leo tubu dhambi zako, msamehe aliyekukosea kabla hujaenda kubatizwa kinyume na hivyo utapoteza muda.
“Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu? Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu”.(Matendo 2:37-38)
Watu wale walipolisikia neno la Mungu lililohubiriwa na Petro walichomwa mioyo yao na walitubu dhambi zao kabla hawajabatizwa.
(iv).Fanya haraka ukabatizwe
Baada ya kulisikia neno la Mungu halafu ukaamini na kutubu unatakiwa kufanya haraka kubatizwa bila kumuuliza shangazi yako, mjomba, dada, kaka, bibi, babu kwa sababu kila mtu atabeba furushi lake mwenyewe.
Kumbuka kwamba ubatizo wa Kibiblia haufanyiki kwa watoto wadogo kwa sababu hawawezi kuisikia injili hivyo hawawezi kuamini. Yesu mwenyewe wakati anafanya huduma hakuwahi kuwabatiza watoto wadogo bali aliwabariki.
“Basi wakamletea watoto wadogo ili awaguse; wanafunzi wake wakawakemea. Ila Yesu alipoona alichukizwa sana, akawaambia, Waacheni watoto wadogo waje kwangu, msiwazuie; kwa maana watoto k**a hawa ufalme wa Mungu ni wao. Amin, nawaambieni, Ye yote asiyeukubali ufalme wa Mungu k**a mtoto mdogo hatauingia kabisa. Akawakumbatia, akaweka mikono yake juu yao, akawabarikia”.(Marko 10:13-15)
Faida za Ubatizo
(i)Kuwa mwana wa utii
Unapokubali kumpokea Yesu kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yako na kubatizwa kibiblia unakuwa mwana wa utii, mtoto anayefuata maelekezo ya wazazi. Kinyume na hivyo utahesabika kuwa mwana wa uasi.
“nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi” (Waefeso 2:1-2)
(ii)Kuonyesha umekufa na Kristo na umefufuka na Kristo
“Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi k**a Kristo alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi tuenende katika upya wa uzima”.(Warumi 6:4)
Unapobatizwa kibiblia unathibitisha kuwa ulizikwa na Kristo na ulifufuka naye. Hivyo ubatizo huu ni jambo la msingi sana kwenye maisha yako.
(iii)Kusamehewa dhambi
(iv)Kufutwa kwa hati ya mashtaka
Je, Mtu Anaweza Kubatizwa Zaidi ya Mara Moja?
Unaweza kubatizwa mara ya pili ulipobatizwa mara ya kwanza ulibatizwa bila kuzamishwa kwenye maji mengi au ulibatizwa ulipokuwa mtoto.
Je Lazima Kubadili Jina Baada ya Kubatizwa?
Jina la mtu ndio mtu mwenyewe!unapobatizwa si lazima ubadili jina lakini k**a jina lako halina maana nzuri na limekuwa chanzo cha matatizo yako nakushauri badilisha baada ya kubatizwa. Mfano unaitwa Matatizo, Majuto, Tabu haya si majina mazuri kwa mustakabali wa maisha yako, vizuri ubadili jina hilo.
MSAADA ZAIDI NA MAOMBEZI:
FIKA KANISANI, UFUFUO NA UZIMA
MKUNDI MWISHO -MOROGORO
AU WASILIANA NASI KUPITIA
FACEBOOK: Ufufuo na Uzima Church Morogoro
Follow us on INSTAGRAM: Ufufuo na Uzima Church Morogoro
Follow us on YOUTUBE: Ufufuo na Uzima Church Morogoro
Email:Ufufuo na Uzima Church [email protected]
TEL: 0719 798 778/0757 550878