19/04/2026
Kristo Yesu anapoingia katikati yao anawauliza swali moja, “Ni maneno gani mnayosemezana hivi mnapotembea?” Yesu anawauliza Mnazungumza nini? Si kwa sababu hajui, bali ili kuwapa nafasi ya kutoa machungu, hofu, na majonzi yaliyokuwa yamejaa mioyoni mwao. Hii inatufundisha kuwa Kristo ni msikilizaji mkuu ambaye anataka tushiriki naye mahangaiko yetu ya kila siku. Kristo anakuja kwetu kila siku, anataka tumweleze yote yanayotusibu k**a hawa wanafunzi walivyomwelezea Yesu masikitiko, hofu, huzuni, kukata kwao tamaa. Kristo anakuja kwetu kila saa ya maisha yetu. Anatupa nafasi ya kumweleza yale yote tunayopitia katika maisha, huenda ni misiba, changamoto za maisha, migogoro ya familia, ni kukata tamaa, udhaifu wetu, mahangaiko yetu ya kila siku katika maisha nk. Ni kweli zipo nyakati tunapitia na hatuoni kabisa tumaini tena. Mara kwa mara katika misiba, katika changamoto kubwa tunaweza kuona namna huzuni inavyojaza mioyo yetu, wakati mwingine tunashindwa kuelewa Neno lolote. Kristo anataka tuseme naye, anatusikiliza. Dominika njema!