11/12/2025
MTUMISHI ZINGATIA HAYA KABLA HUJAANZA HUDUMA
1. Huduma inahitaji Uvumilivu. Usiwe mwepesi kukata tamaa.
2. Haijalishi umeanzaje lakini jiandae kwa nyakati za kupimwa na kujaribiwa katika huduma yako.
3. Huduma itachanua kwa kuzingatia kutembea na Mungu, uaminifu, kutochoka mapema.
4. Kila hatua ya huduma ina watu wake na marafiki wake. Kuna wakati watu fulani watakuja au wataondoka. Usiwe mwepesi kujisahau kwa wanaokuja au kulaani wanaoondoka kipindi chao kinapoisha.
5. Hakikisha huduma yako ina mlezi au msimamizi wa kiroho anayeweza kukukemea na kukukosoa na ukanyenyekea na kusikiliza.
6. Unapopata fursa ya kutumika mahali tumika kwa moyo na nguvu zote maana huwezi kujua hiyo fursa moja itakufungulia milango gani.
7. Usikimbilie kuiga wanachofanya wengine na kikawasaidia kwenye huduma zao, kabla hujatulia na kuomba uongozi wa Roho Mtakatifu k**a na wewe kitakufaa.
8. Kuna watumishi wengine wa Mungu kamwe hawatatambua wito wako wala kukukubali. Usipambane nao.
9. Kuna watumishi tena marafiki zako watabebea bango madhaifu yako na kamwe hawataangalia alichoweka Mungu ndani yako. Songa mbele.
10. Unahitaji kujijengea nidhamu ya hali ya juu katika Neno la Mungu na kujilinda na mawaa ili utumishi wako usiwe wa kulaumiwa.
11. Heshimu walio mbele yako kihuduma bila kujali umri wao.
12. Ushindani ni mkubwa. Kuwa na hekima, mbinu na shindana kwa msaada wa Mungu.
13. Katika huduma yako kitu kingine chochote kisiwe na thamani zaidi kuliko roho au nafsi ya mtu.
14. Ikimbie zinaa, pombe, tamaa (ya mwili, ya macho, ya mali), masengenyo, wivu na kiburi cha uzima.
15. Tunza sana siri zako na siri za waumini wako.
16. Kila mwaka kuna waumini wako unaowategemea sana wataondoka. Ila Roho Mtakatifu na vipawa alivyokupa havitaondoka.
17. Hakuna mjadala kuhusu Kufunga na Kuomba kila mara ili huduma yako ichanue.
18. Unyenyekevu utakuinua hata pale wengine wanapoona huna vigezo.
19. Usiendekeze sana kukaribishwa kwenda kuhudumia makusanyiko mengine kuliko kulihudumia kundi ambalo utalitolea hesabu.
20. Wapende na wajali washirika wako. Watie moyo, watembelee na ulizia maendeleo yao.