23/02/2025
SIKU 3 ZA KUFUNGA NA KUOMBA.
KUSHUGHULIKA NA MIUNGANIKO YA KIROHO-GIZA
SEHEMU YA KWANZA: MIUNGANIKO YA KIROHO-GIZA
“Lakini yeye aliyeungwa na Bwana ni roho moja naye.” 1 Wakorintho 6:17
Katika ulimwengu wa roho, unaweza kuungana na Bwana na ukawa roho moja naye au pia unaweza kuungana na nguvu za giza. Bwana Yesu alipotuokoa alikusudia tuungane naye, ili tuweze kuishi maisha ya ushindi, maisha yenye msaada kutoka kwake na tuweze kuzaa matunda yapasayo toba, maana bila Yeye sisi hatuwezi kitu (Yohana 15:5).
Ni wazi maisha ya wokovu bila muunganiko na Bwana, yanakosa matokeo halisi ya wokovu. Pengine maisha ya namna hiyo ni maisha fulani yanayotaka kufananishwa na wokovu lakini si maisha halisi ya wokovu uliokusudiwa na Bwana wetu Yesu Kristo.
Kuungana na Bwana hapa ninazungumza juu ya maisha ya kutembea katika neno la Mungu yaani neno linaongoza matendo yako, maneno yako na mara nyingine mawazo yako. Mtu wa namna hii anaishi ndani ya Yesu, au kwa lugha nyingine ameungana na Bwana na ni roho moja naye, na huyu ndiye mtu huzaa sana.
Sasa katika ulimwengu wa roho kuna pande mbili, upande wa nuru na upande wa giza. Upande wa nuru ni upande wa Bwana, na upande wa giza ni upande wa adui au shetani. K**a hujaungana na Bwana umeungana na upande wa shetani kupitia matendo yako, au matendo ya wahenga wako, kwa kujua au kwakutokujua.
Hivyo kule kuungana na nguvu za giza ndiko tunaita ‘miunganiko’ au ‘fungamano’ la kiroho-giza. Ninapozungumza kuhusu fungamano nina maanisha njia au mlango ambao shetani hutumia kuingiza uharibifu katika maisha ya mtu au katika familia yake. Maana pasipo fungamano shetani hawezi kupata ‘access’ ya kuingia katika maisha ya mtu.
Kwa hiyo unaweza ukawa ndani ya kanisa au wokovu lakini una fungamano la siri ambalo linakuunganisha na nguvu za giza bila wewe kujua. Kwa sababu shetani hufanya kazi kwa siri ili kuzuia asijulikane. Mtu atashangaa tu, anapita katika vita kubwa ya kiroho isiyoisha katika maisha yake. Ataomba sana, atafunga sana na mara nyingine atatoa sadaka sana lakini hakuna kinachobalika.
Shida hapa sio maombi, ama mfungo ama sadaka unazotoa ila ni fungamano ulilonalo. Linalotoa uhalali kwa shetani. Kwa lugha nyepesi una ‘kitu cha adui ndani kwako’, na hicho kitu ndiyo tunaita ‘fungamano’. Sasa Mungu ametupa neema ya kufunga na kuomba kwa ajili kujiondoa katika haya mafungamo, maana yake ametupa fursa ya kuondoa hivi vitu vya adui maisha ni mwetu ili tuweze kuwa na muunganiko uliosawa na Bwana.
Ni yangu imani kwamba katika maombi haya, Mungu atakwenda kuvunja na kukata kila miunganiko tulionayo na adui, tuliojiunganisha kwa kujua au kwakutokujua. Ndipo watu wengi katika mfungo huu wataweza kuvuka katika vita visivyoisha wanavyopigana kiroho. Weka imani kwa Mungu na bila shaka unakwenda kufunguliwa. Hongera kwa mfungo siku ya kwanza.
MAOMBI YA ASUBUHI NA JIONI.
1. Mshukuru sana Mungu kwa ulinzi, afya, na maisha yako kwa ujumla; pia mshukuru sana Mungu kwa kukuwezesha kushiriki mfungo huu wa siku tatu. (1 Nyakati 16:34)
2. Omba toba mbele za Mungu kwa matendo yote yasio mema uliowahi kutenda au yaliyotendwa na wazazi wako na yakakuunganisha na ufalme wa giza, k**a uchawi, ushirikina, uganga, matambiko, mazindiko, ibada za mizimu, uaguzi, zinaa, uganga wa kuchanjwa chale, na mengine unayoyakumbuka. (Yakobo 5:16)
3. Jiondoe kwa kutumia damu ya Yesu kwenye kila muunganiko wa kiroho-giza uliopo. (1 Kor 6:17)
4. Muombe Mungu akupe neema ya kuishi maisha ya muunganiko naye daima yaani neema ya kuishi sawasawa na neno lake siku zote ili: (Yohana 15:4-7)
• Uweze kuishi maisha yenye matunda (uzae sana)
• Uweze kutimiza kusudi uliloumbiwa
• Usije kutupwa nje kweney maisha ya mateso
• Uweze kuomba lolote kwa Mungu na ukapokea.
5. Ombea sana huduma hii ili iweze kufikia watu wengi zaidi katika maeneo zaidi k**a ilivyokufikia, pia niombe mwalimu wako ili Mungu anitunze siku zote kwa ajili ya kazi hii yake.