UPAKO WA OMEGA

UPAKO WA OMEGA Ukurasa huu unahusika zaidi na Kuhubiri Injili ya Bwana Yesu Kristo na kuutangaza Ufalme wa Mungu. Lakini pia mambo mbalimbali ya kijamii.

09/06/2021

NAMI NIENDAKO MWAIJUA NJIA.

"4. Nami niendako mwaijua NJIA. 6 Yesu akamwambia, Mimi ndimi NJIA, na kweli, na uzima; MTU HAJI KWA BABA ILA KWA NJIA YA MIMI"(YOHANA 14:4,6).

Katika mistari iliyotangulia kabla ya wa 4,yaani YOHANA 14:1-3,Bwana Yesu alianza kuwaambia wanafunzi na wafuasi wake; "Msifadhaike mioyoni mwenu... Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; k**a sivyo ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali. Basi Mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo Mimi, nanyi mwepo". Katika mistari hii kimsingi alikuwa anasema anakwenda Mbinguni au Peponi kwenye Makao ya Furaha na raha tele. Halafu ndipo ukafuata huo mstari wa 4; "NAMI NIENDAKO(yaani huko Mbinguni) MWAIJUA NJIA". Katika mstari wa 5 Mwanafunzi Tomaso akamwomba Bwana awafahamishe bayana juu ya hiyo NJIA. Ndipo mstari wa 6 Bwana Yesu akatanabaisha bila chenga juu ya NJIA hiyo ya kwenda Mbinguni; "Yesu akamwambia, Mimi ndimi NJIA, na kweli, na uzima; MTU HAJI KWA BABA, ILA KWA NJIA YA MIMI".

Wengi wetu tunafahamu juu ya Njia. Njia ni kiongozi yaani hutuongoza kufika kule tulikokusudia kufika/kwenda.
Duniani zipo njia za namna mnalimbali ambazo kwazo mtu huweza kufika kule aendako. Mtu akitaka kwenda kazini, shambani au kwenye shughuri zake za kila siku sharti aifuate njia ya kwenda huko. Iwapo mtu anataka kurudi nyumbani kwake au pale anapoishi, sharti aifuate njia ya kwenda kwake. Ipo njia ya kwenda sokoni, dukani, bombani au kisimani, Kanisani au kwenye nyumba ya ibada nk.
Ili mtu aweze kufika kule alikoazimia kwenda/kufika ni lazima aifuate njia sahihi ya kumfikisha huko. Iwapo mtu ataamua kuifuata njia yoyote ilimradi itakuwa vugumu sana kufika kule alikoazimia kufika. K**a mtu yupo DSM na anataka kufika Arusha sharti aifuate njia ya kwenda Arusha; k**a ataamua kuifuata njia iendayo Mbeya au Mtwara ni vigumu kwa mtu huyo kufika Arusha. Kwanini? Kwa sababu hakuifuata njia sahihi iendayo Arusha.

Vyivyo hivyo ipo NJIA ya kwenda Mbinguni. Ili mtu aweze kufika Mbinguni ni lazima aifuate NJIA sahihi ya kwenda Mbinguni. K**a mtu ataamua kufuata njia yoyote ilimradi kwa matarajio ya kufika Mbinguni, kamwe hataweza kufika huko.
Tofauti na hapa duniani, mtu anaweza kufika mahali fulani kwa kutumia njia tofauti tofauti; lakini katika suala zima la kufika Mbinguni NJIA IPO MOJA TU. Hapa duniani mtu anaweza akafika mahari fulani kwa kutumia usafiri wa Gari yaani njia ya barabara; lakini anaweza kuamua kutumia Treni au gari moshi yaani njia ya reli; au anaweza akapanda Ndege kwa njia ya anga :katika mazingira mengine akaamua kupanda Meli au boti kwa njia ya majini. Lakini linapokuja suala la kwenda Mbinguni NJIA ipo moja tu nayo ni Bwana Yesu Kristo; "MTU HAJI KWA BABA ILA KWA NJIA YA MIMI" asema Bwana Yesu. Katika MATENDO YA MITUME 4:12,Biblia inasema; "Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo". Ni Jina la Yesu Kristo pekee ndipo tunapoweza kuhesabiwa haki na kupata wokovu wa roho zetu. Mistari iliyotangulia anatajwa kuwa ni Jiwe lilikataliwa na waashi ambalo ni Jiwe Kuu la pembeni.

Mpendwa msomaji, je ungependa kufika Mbinguni, kwenye Makao ya milele? Huyu Yesu ndiyo NJIA. Ukitubu dhambi zako na kumpokea Yesu Kristo k**a Mwokozi na Bwana wa maisha yako utakuwa unatembea katika Njia ya Uzimani/Mbinguni. Damu Yake ya thamani kuu itakusafisha kabisa. Jina lako litafutwa kwenye kitabu kimojawapo cha Hukumu na kuandikwa kwenye Kitabu cha Uzima cha Mwanakondoo. Utahesabiwa haki bure ya kuingia Mbunguni nk nk. K**a upo tayari fuatisha sala hii ya kutubu dhambi na kuokoka. Sema: "BWANA YESU, NIOSHE KWA DAMU YAKO. NAKUPOKEA K**A MWOKOZI NA BWANA WA NAISHA YANGU. KATIKA JINA KUU LA BWANA YESU AMEN". Tayari. Jiunge na kanisa la wokovu kwa msaada zaidi. Kwa maulizo au msaada zaidi wa kiroho unaweza kunipigia kwa Simu/WhatsApp 0783 75 26 31(+255 783 752 631). Ndimi ndugu yako Pastor Sume Mbena.

29/05/2021

NITAKUJA TENA NIWAKARIBISHE KWANGU.

"Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; k**a sivyo ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali. Basi Mimi nikienda na kuwaandalia mahali, NITAKUJA TENA NIWAKARIBISHE KWANGU; ili nilipo nanyi muwepo"(YOHANA 14:2-3).

Maneno haya aliyasema Bwana Yesu Kristo, muda mchache kabla ya kupaa na kwenda Mbinguni.
Hii ni Ahadi aliyoitoa Bwana Yesu kwa wafuasi wake; kila aliyetubu dhambi zake na kuokolewa, kisha kumuishia Kristo; ambaye dhambi zake zimeoshwa kwa Damu ya Mwanakondoo(Yesu Kristo) aliyechinjwa tangu kuwekwa misingi ya ulimwengu.

Katika mistari hiyo kuna mengi ya kujifunza, lakini katika Makala hii tutayaangalia zaidi maneno haya "NITAKUJA TENA NIWAKARIBISHE KWANGU". Kwake Yesu Kristo ambapo pia ni kwa Baba Yake ni Mbinguni. Hivyo atakuja tena atukaribishe Mbinguni, kwenye Makao ya milele yaliyotukuka! Lakini itakuwaje hasa?

Hivi ndivyo itakavyokuwa. Kwa ghafla, kufumba na kufumbua, pasipo taarifa yoyote, huku shughuri za dunia zikiendelea k**a kawaida; Parapanda ya Mungu italia, ila Parapanda hii haitasikiwa na isiyowahusu bali itasikiwa na wale watakaonyakukuliwa tu. Kisha wafu waliokufa katika Bwana tangu nyakati za Adamu watafufuliwa. Waliokufa katika Kristo tu, wafu wengine wataendelea kubaki huko Kuzimu. Kisha sisi wengine tulio hai tutaungana na hao walionyakuliwa kwenda kumlaki Bwana Yesu Mawinguni, mbali sana kule juu asipoweza mtu kuona. 1WATHESALONIKE 4:15-17 Biblia inasema hivi; "Kwa kuwa tunawaambia haya kwa neno la Bwana, kwamba SISI TULIO HAI, TULIOSALIA HATA WAKATI WA KUJA KWAKE BWANA, hakika hatutawatangulia hao waliokwisha kulala mauti. Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka Mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya Malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. KISHA SISI TULIO HAI TULIOSALIA, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele".

Zipo imani za dini nyingine zinazofundisha "kila nafsi itaonja mauti"; lakini Biblia yangu inasema wakati wa kuja Bwana wapo watu watanyakuliwa wakiwa hai. Katika maandiko niloyosoma hivi punde nimeyaandika kwa herufi kubwa ili kukuonyesha hilo. Mahali pengine Biblia inasema hatutalala sote yaani hatutakufa sote bali sote tutabadilishwa. Yaani pale tunaponyakuliwa miili hii ya unyonge na uharibifu itabadilishwa na kuchukua miili mipya k**a ya Almasi hivi tutakayoishi nayo milele Mbinguni. Angalia 1KOR 15:51-52; "Angalieni, nawaambia ninyi siri; HATUTALALA SOTE, lakini sote tutabadilika, kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa Parapanda ya mwisho, maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika".

Kwa hiyo hili ndilo Tumaini letu kuu, kwa kila mfuasi wa kweli wa Yesu Kristo. Ya kwamba Bwana atakuja kutuchukua k**a alivyoahidi. Na bila shaka wakati huo umefika, tunamtarajia Bwana sekunde yoyote dalili za nyakati zinaonyesha hivyo. Tunamtazamia Mwokozi. WAEBRANIA 9:28 inasema, "Kadhalika Kristo naye; akiisha kutolewa sadaka mara moja azichukue dhambi za watu wengi; ATATOKEA MARA YA PILI PASIPO DHAMBI, KWA HAO WAMTAZAMIAO KWA WOKOVU". Na katika WAFILIPI 3:20-21 tunasoma; "Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko Mbinguni; kutoka huko tena(Mbinguni) tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo; ATAKAYEUBADILI MWILI WETU WA UNYONGE, UPATE KUFANANA NA MWILI WAKE WA UTUKUFU".

Watakaonyakuliwa na kumlaki Bwana Yesu Mawinguni ni wale waliotubu dhambi zao na kuokolewa. K**a bado hujampokea Yesu na kuokoka hautakuwemo miongoni mwa watakaonyakuliwa, haijalishi unashika dini kiasi gani. Lakini pia si wote wanaosema wamwokolewa watakaonyakuliwa, Vuguvugu yaani wanaoituatisha namna ya dunia hii iwe katika mavazi, mapambo nk hawatanyakuliwa; haijalishi utumishi mtu anaoufanya au inaonekana tupo karibu na Mungu sana akijibu maombi yetu au karama yoyote tuliyonayo au jinsi Mungu anavyotutumia. Labda wakati mwingine nitafafanua hili, maana kuna kudanganyika sana watu wakidhani kutumiwa na Mungu ndiyo kibali cha kuingia Mbinguni, tofauti kabisa! Wanafiki yaani wakristo bandia, walokole bandia, wachungaji bandia nk nao hawatajenda. Nikitaka kusema ukwelI, kwa jinsi inavyoonekana yaani hali ya kiroho iliyopo ya watu waliookoka leo, watakaonyakuliwa watakuwa wachache sana!
Mara baada ya Unyakuo Dunia itashikwa na Shetani kwa muda; utakuwa ni wakati wa mashetani kuwatesa wanadamu mubashara. Kwa miaka saba Mpinga Kristo chini ya Utaratibu mpya wa Dunia yaani New Word Order atatawala. Kwa kweli itakuwa ni zaidi ya hatari.
Tafakari. Chukua hatua. Wakati wa wokovu ni sasa. Ndimi ndugu yako Pastor Sume Mbena wa Huduma ya PENUEL, DSM. (+255 783 752 631).

30/04/2021

JINSI YA KUUKOMBOA WAKATI - SEHEMU YA 6.

Katika sehemu iliyopita nilimalizia kwa kusema, KUUKOMBOA WAKATI ni kutumia Wakati/Muda wetu na Wakati uliopo katika kutekeleza KUSUDI la Mungu kwetu kwa Wakati wake.

Katika kitabu cha MATENDO YA MITUME 13:36,anatajwa Mfalme Daudi; "Kwa maana Daudi,akiisha kulitumikia KUSUDI la Mungu katika kizazi chake akalala... ". Ukiyaangalia vizuri maneno hayo utagundua, yana maana kuwa Kulitumikia yaani kulitekeleza au kulitimiza KUSUDI la Mungu kwa Daudi, ndiyo sababu hasa ya kuishi kwake au yeye Daudi kuwepo/kuja duniani. Na alipokwisha kulitumikia akalala mauti, yaani kazi aliyotumwa kuifanya ameimaliza kwa kadiri alivyoweza.

KUSUDI la Mungu katika maisha yetu ndiyo sababu ya sisi kuwepo duniani. Hekima ya Mungu ni kulitumikia au kulitekeleza KUSUDI hilo kwa Wakati wake. Kwa hiyo ili tuweze Kuukomboa wakati ni lazima kwanza tulifahamu KUSUDI hilo na kisha tutumie Muda tulio nao kulitekeleza/kulitimiza.

KUSUDI la Mungu katika maisha yetu ndiyo nini hasa? Na tunawezaje kulitambua? Kusudi la Mungu kwetu ni jambo, shughuri au jukumu tulilopangiwa na Mungu kulifanya hapa duniani. Yapo Makusudi tofauti tofauti kutoka mtu mmoja hadi mwingine. Pia hutokea kufanana.

Nimeshaeleza kwamba sisi tumetoka kwa Mungu. Kuja kwetu hapa duniani siyo bahati mbaya. Hata k**a inaonekena mimba ilitungwa kwa bahati mbaya, yaani wazazi wote au mmoja, hawakupanga kupata mtoto kwa muda huo, lakini kuja kwa mtu(roho) siyo bahati mbaya kamwe, bali ni mpango kamili wa Mungu.
Jambo la kufahamu ni hili, kila mtu anapokuja duniani anakuwa amebeba KUSUDI au kazi fulani maalum ya kuitekeleza hapa duniani.
Inavyoonekana mara tutokeapo duniani yaani pale tunapozaliwa KUSUDI lile tunalisahau! Hiyo haina maana hatujapewa KUSUDI. Kazi hiyo maalum au KUSUDI tulipewa KABLA mimba yetu haijatungwa yaani pale tulipokuwa tunatoka kwa Mungu! Embu sikiliza kile Mungu alichoongea na Yeremia, na ndivyo ilivyo kwa kila mmoja wetu; YEREMIA 1:4; "Neno la BWANA lilinijia kusema, KABLA sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatokea tumboni nalikutakasa; NIMEKUWEKA KUWA NABII WA MATAIFA". KUSUDI la Mungu kwa Yeremia la kuwa Nabii wa Mataifa, alipewa KABLA hajatungwa mimba! Hapo Mungu alikuwa anamkumbusha tu, na ndicho tunachopaswa kumuomba Mungu afanye kwetu; na mara baada ya Yeremia kukumbushwa kazi ilikuwa moja tu kulitumikia au kulitekeleza Kusudi hilo.

Ndiyo maana ni muhimu sana kwa kila mmoja wetu kulifahamu KUSUDI la Mungu katika maisha yake hapa duniani, vinginevyo hatutaweza kamwe Kuukomboa wakati maana tutakuwa tunafanya mambo tusiyopangiwa na huko ni kupoteza wakati hata k**a mambo hayo ni mazuri na yana manufaa. Faida nyingine ya kulifahamu KUSUDI la Mungu kwetu ndipo tutakapopata Muelekeo sahihi juu ya maisha yetu. Lakini pia itatusaidia kufanya Maamuzi sahihi na thabiti maana si tunajua yatupasayo kufanya? Na muelekeo tunaufahamu. Hivyo hatutayumba yumba mara tufanyapo maamuzi hasa maamuzi magumu. Lakini pia tutaweza kuweka vipaumbele katika maisha haya, hiyo ni pamoja na matumizi ya muda wetu, rasilimali zetu,nguvu zetu nk.

Kusudi la Mungu katika maisha yetu ndilo linapaswa kuongoza maisha yetu yote hapa duniani. Mahali tutakapoishi, aina ya mwenzi, na kila jambo tunalolifanya liwe kubwa au dogo! Kwanini? Kwa sababu jambo lolote tunalolifanya linatuchukulia muda wetu yaani linakula muda tulionao iwe sana au kidogo. Kwa hiyo vitabu au magazeti tunayosoma; watu tunaowatembelea au marafiki zetu au chochote kingine. Yule tunayemuita rafiki lakini anakwepa kuchangia Kusudi letu kwa namna ama nyingine k**a sisi tulivyo tayari kuchangia Kusudi lake;tumuache aende hata k**a tulimpenda sana.
Paulo mtume aliposema, "...ila natenda neno moja tu... ",si kwamba alikuwa hafanyi jambo jingine lolote, la hasha! Bali kila jambo alilokuwa akilifanya pamoja na kushona mahema lilikuwa kwa ajili ya jambo moja tu, kutekeleza Kusudi la Mungu katika maisha yake. Kusudi hilo ameliongea mara kadhaa kwa namna tofauti tofauti, kwa mfano katika 1TIMOTHEO 2:7 anasema, "Nami kwa ajili ya huo NALIWEKWA NIWE MHUBIRI NA MTUME... MWALIMU WA MATAIFA katika imani na kweli". Hivyo lolote alilokuwa analifanya, na popote alipokuwa anakwenda alikuwa ni kwa ajili ya Kusudi hilo, hata mahali pengine akasema anafanya mambo YOTE kwa ajili ya Injili ili kuishiriki na wengine. Huko ndiko Kuukomboa wakati, yaani kufanya jambo lolote ikiwa tu linachangia kwa namna moja ama nyingine kutekeleza Kusudi la maisha yetu; na lile lisilochangia tunaachana nalo hata k**a tunafikiri ni jema na lina manufaa fulani. Kumbuka KUSUDI la Mungu katika maisha yetu ndilo linalopaswa kuongoza maisha yetu hapa duniani maana wakati unakuja tutakapotakiwa kutoa hesabu jinsi tulivyotekeleza. Katika Siku ya kutoa hesabu kutakuwa na mambo au masuala mawili ya kujieleza au yatakayokaguliwa, la kwanza ni kuhusu Wokovu wetu katika Mwanawe Yesu Kristo, na maisha yetu ya uchaji, na la pili kuhusiana na kazi, jukumu au utumishi ule aliotuitia duniani ,tumeutekelezaje? Na jinsi tulivyotumia talanta mbalimbali alizotupa kwa utekelezaji wa jukumu hilo vikiwemo vipawa vya asili, karama na neema mbalimbali.

Kuna jambo ambalo nilitamani au nilipanga kuliongelea katika sehemu hii, lakini muda si rafiki. Tukutane katika sehemu ijayo kwa neema ya Mungu kwa muendelezo wako. Ni mimi ndugu yako, mtumwa wa Bwana Yesu Kristo, Mch Sume Mbena wa Huduma ya PENUEL. Mungu akubariki.

16/04/2021

JINSI YA KUUKOMBOA WAKATI - SEHEMU YA 5.

"Kwa KILA JAMBO kuna majira yake,
Na Wakati kwa KILA KUSUDI chini ya Mbingu.
WAKATI WA KUZALIWA, NA WAKATI WA KUFA; " (MHUBIRI 3:1-2a).

WAKATI WA KUZALIWA ndiyo lango la kuingilia duniani kutokea huko tulikotoka yaani kwa Mungu. Hapa ninazungumzia roho ya mtu ambayo ndiyo mtu halisi, mtu wa ndani. Mwanadamu awapo duniani ana roho, nafsi na mwili. Mwili ndiyo nyumba ya roho, ndiyo unaotuwezesha kuishi hapa duniani (2WAKORINTHO 5:1-4). Mtu anapokufa roho na mwili vinatengana kinachobaki ni mwili wa fulani, lakini fulani mwenyewe anakuwa ameondoka. Mwili unarudi mavumbini maana ndiyo asili yake, lakini roho inapaswa kurudi kwa Mungu maana ndiko ilikotoka(MHUBIRI 12:7).
Roho ya mwanadamu huwa pamoja daima. Nafsi hujumuisha fikra, hisia, kumbukumbu, akili, utambuzi wa mambo na mambo yanayofanana na hayo. Maneno mbalambali kwenye Biblia hutumika kuzungumzia kitu hicho hicho Nafsi ya mwanadamu, baadhi ya maneno hayo ni Fikra, Nia nk. Adui Ibilisi anapotaka kumdhibiti mwanadamu, kumfanya awe mbali na Mungu na kumuongoza kusiko sahihi huwa anashambulia Nafsi ya mwanadamu. Maandiko yanaeleza mtu ambaye hajaokoka ni kwa sababu Nafsi/Fikra zimetiwa upofu na Mwovu Shetani ili wasione Njia sahihi ya Uzima wa milele (2 KOR 4:3-4; WAEFESO 4:17-19).

K**a nilivyotangulia kusema, roho ya mtu ambayo ndiyo mtu halisi/mwenyewe inatoka kwa Mungu. YOHANA 1:6 inasema; "Palitokea mtu AMETUMWA KUTOKA KWA MUNGU, jina lake Yohana". Huyu ni Yohana mbatizaji. Katika Biblia ya kiingereza mstari huo unasomeka hivi; "There was a man SENT FROM GOD, whose name was John". Ametumwa kutoka kwa Mungu. Lakini tunajua kwamba Yohana amezaliwa na mama yake aitwaye Elizabeth, na babaye ni Zakaria wa zamu ya Abiya sasa imekuwaje awe America kwa Mungu?
Iko hivi, muda ule ule mimba inapotungwa, yaani mbegu kuingia kwenye Yai ndani ya tumbo la uzazi, sekunde ile ile Bwana Mungu huituma roho(Mtu) kutoka Mbinguni na kuingia ndani ya Yai hilo. Kimsingi tangu sekunde ile ya kwanza mimba inapotungwa ni kiumbe hai, namna yoyote ya kutoa ni uuaji k**a ulivyo uuaji mwingine. Mwili unatokana na baba na mama, lakini roho inatoka kwa Mungu.
Kwa hiyo Bwana Mungu kila siku hutuma roho huku na huko duniani kote, mimba zinapotungwa. Bwana Mungu ndiyo uamua mtu fulani azaliwe wapi, katika Taifa lipi na kabila gani, achukue mwili wa jinsia gani, achukue mwili wa rangi gani? Wazazi wake wawe akina nani nk. Kulingana na makusudi yake.
Wanadamu tunapobaguana kwa ajili ya rangi ya miili yetu ni ujinga kupindukia. Roho ya mtu haina rangi hizi. Pia mtu(roho) angeweza kuzaliwa popote na kuchukua mwili wa rangi na taifa lingine tofauti na tulivyo sasa. Hata miili ya Mbinguni ile ya utukufu ni tofauti kabisa na hii; ile ni k**a ya Almasi hivi wala siyo ya kizungu, kichina, kihindi, kiarabu wala kiafrika.
Pia ni ulimbukeni wa kutisha kujivunia miili hii, maandiko yanasema mwili wa damu na nyama, kwa jina lingine uharibifu haiwezi kurithi kutokuharibika yaani Uzima wa milele. Miili hii tamati yake ni kwenye udongo basi. Ila ni jambo zuri kuilinda na kuitunza ili isiharibike, maana kwa hii ndiyo inatuwezesha kuishi hapa duniani na kukamilisha makusudi mbalimbali ya Mungu tuliyotumwa kwayo. Ikiharibika kwa namna yoyote ile, iwe kwa magonjwa, ajali, kupigwa, sumu au uharibifu wowote mkubwa, roho haiwezi tena kukaa ndani yake inabidi kuondoka.

Kwa hiyo sasa WAKATI WA KUZALIWA ndiyo Wakati wa sisi kuja duniani, ndiyo mlango wa kuingilia ulimwenguni. Lakini pia WAKATI WA KUFA ndiyo mlango wa kutokea yaani wa kuondokea duniani, na kwenda mahali fulani aidha Uzimani au Kuzimu Mautini. Hilo siyo ninalotaka kulizungumza kwenye Makala hii.

Kati ya WAKATI WA KUZALIWA na WAKATI WA KUFA, kuna Muda hapo katikati, huo ndiyo unaitwa WAKATI WETU. WAKATI WETU ni Muda uliotolewa au uliopangwa na Mungu wa mwanadamu kuishi duniani kwa ajili ya jambo au KUSUDI fulani. Wakati huu utofautiana tofautiana kutoka mtu mmoja hadi mwingine,maana watu wa rika zote hufa. Na mtihani mkubwa aliopewa mwanadamu ni jinsi gani anautumia Muda wake duniani.
Jambo la kufahamu ni hili, tangu Wakati ule tulipozaliwa, sina hakika k**a tangu Wakati ule tulipoingia tumboni; yupo Mtu asiyeonekana anaeanza kuhesabu muda wetu (Time keeper) tunaoutumia, na muda ule tuliopangiwa ukikamilika tu basi ujue kuondoka ni lazima tuondoke, hakuna kufanya ujanja wala kukwepa.
Kila sekunde inayokwenda ujue ndiyo tunakula muda wetu tuliopewa kuishi hapa duniani, ndivyo Muda/Wakati wetu unavyozidi kupungua na kuisha. Muda wangu sijui umebaki kiasi gani? Je wewe mpendwa, unadhani Muda wako umebaki kiasi gani? Kwa vyovyote vile Muda wetu umebaki mchache sana, maana maandiko yanasema mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake si nyingi. Na tena siku hizo zinakwenda kwa kasi sana.

Lakini kuna jambo la ziada ambalo ndilo hasa nataka nilisisitize. Kuja kwetu hapa Duniani tumetumwa kutoka kwa Mungu, kwa ajili ya KUSUDI/Kazi maalum k**a tu ilivyokuwa kwa Yohana Mbatizaji. Makusudi au Kazi tuliyoitkwa kufanya ni tofauti tofauti kutoka mtu mmoja hadi mwingine. Jambo kuu ni kwamba KILA KUSUDI limepangiwa Muda wake wa kukamilishwa. Kwa hiyo kwa mtazamo wangu KUUKOMBOA WAKATI ni kulitumikia KUSUDI tulilopewa kwa Wakati wake. Ni kukamilisha kazi tuliyopangiwa na Mungu kufanya hapa duniani sawa na Muda uliotolewa kwa KUSUDI hilo. ITAENDELEA.

13/04/2021

JINSI YA KUUKOMBOA WAKATI - SEHEMU YA 4.

"Kwa KILA JAMBO kuna majira yake,
Na Wakati kwa kila Kusudi chini ya Mbingu". (MHUBIRI 3:1).

K**a utachoma moto karatasi au lundo la nyasi, bila shaka kiasi fulani cha MUDA kitatumika Hata kufikia karatasi au nyasi hizo kuteketea na kuwa majivu. Kiasi hicho cha muda kilichotumika tunaweza kukiita Muda wa kuteketea kwa karatasi au nyasi.
Mtu fulani anaweza akaniambia ya kwamba kiasi cha Muda utakaotumika itategemeana na kiasi cha moto kinachounguza karatasi au nyasi hizo.Hiyo kimantiki ni kweli. Lakini kuna ukweli zaidi ya huo usiojukikana, ya kwamba Muda/Wakati ndiyo unaamua karatasi au nyasi hizo ziteketee hata kuwa majivu!
Eti nini? Ndivyo ilivyo. Katika kitabu cha KUTOKA 3:1-3,Musa akiwa machungoni, aliona kijiti(kichaka) kinawaka moto lakini hakiteketei! Yaani hakimaliziki na kuwa majivu. Unafahamu nini kilichotokea pale? Mungu Mwenyezi aliondoa Muda ndani ya kichaka kile;na hivyo ule Muda wa kuteketea ukakosekana, hiyo ndiyo sababu kchaka kikawa kinaungua pasipo kuteketea!

Ni kwamba, Muda/Wakati ndiyo unaotawala,kuongoza au kudhibiti mambo na vitu mbalimbali chini ya Mbingu yaani duniani hapa. Ikiwa wakati/muda utandolewa juu ya kitu basi hukaa hali ile ile au hiyo hiyo.

Katika kitabu cha Yoshua tunamuona Mtumishi wa Mungu Joshua akilisimamisha jua juu ya Gibeon pia mwezi usichomoze! Ikawa hivyo! Ni wazi Mungu Mwenyezi alisimamisha Muda katika Dunia nzima kwa siku nzima! Mchana uliendelea kwa takribani masaa 24 mengine!

Wakati fulani nilihudhurua Semina ya Mtumishi mmoja wa Mungu, mzungu kutoka Marekani. Akaeleza wakati fulani alikuwa Nchini Cambodia kulikokuwa na vita vya ndani na machafuko. Alikwenda huko kwa ajili ya Injili na kutoa misaada ya kibinadamu. Hali ilikuwa mbaya sana, pia kulikuwa na njaa sana. Kwa hiyo wakawa wanagawa chakula kwa msululu wa watu Wahitaji waliokuwa wamepanga foleni. Yeye akikuwa anagawa matunda aina ya matikiti. Alikuwa anakata vipande na kugawa. Lakini watu walikuwa wengi sana kiasi kwamba yale matikiti yasingeweza kabisa kutosha hata kidogo. Jambo la ajabu likatokea, akagundua kila tikiti lilikuwa linachukua muda mrefu kumalizika kuliko kawaida! Labda k**a ingechukua dakika mbili kumaliza kulikata tikiti na kugawa, sasa ichukue dakika labda kumi! Matokeo yake wote walipata tikiti mpaka kubaki! Ni muujiza! Lakini unajua kilichotokea? Bwana Mungu alizidisha muda wa kumalizika kukatwa kwa tikiti. Bila shaka k**a angeondoa muda kabisa kwenye tikiti basi lingekatwa pasipo kumalizika.

Bila shaka utakuwa unakumbuka muujiza ule, pale Bwana Yesu alipowalisha watu maelfu kwa mikate mitano na samaki wawili? Unajua nini kilichotokea katika muujiza ule? Mungu Mwenyezi aliondoa au kuongeza muda katika mikate na samaki wale. Hivyo vikimegwa haviishi! Watu wakala, wakashiba hadi wakasaza!

Nachotaka kusema hapa ni kwamba Muda(Wakati) ni kitu cha ajabu sana Bwana Mungu alichokiumba. Bwana Mungu ameweka Muda ili kuongoza na kudhibiti vitu na mambo mbalimbali huku chini ya Mbingu.

Bila shaka sasa unaweza kuelewa, kwanini Mungu ni wa milele? Ni kwa sababu Yeye hadhibitiwi na Muda/Wakati bali kinyume chake Yeye ndiye anayeudhibiti Wakati/Muda,na ndiye akiyeuumba!

Bila shaka sasa unaweza kuelewa nini maana ya maisha ya milele? Ni kwa sababu Muda/Wakati utaondolewa usiwepo tena. Katika umilele Muda hauhesabiwi tena.Katika maisha yale yajayo iwe Mbinguni au Motoni kutakuwa hamna kitu kinachoitwa Muda au Wakati. Maandiko yanasema, Malaika mwenye nguvu akapaza sauti yake "Hakutakuwa na Muda baada ya haya ".

Hata hivi sasa Mbinguni hakuna kitu kinachoitwa Muda. Mbinguni Hakuna dakika, saa, siku wala sijui mwaka.
Kabla ya uumbaji wa ulimwengu Muda haukuwepo, bali alikuwepo Mungu Mwenyezi aliyekuwepo tangu milele, ambaye hana mwanzo wa siku zake. Muda uliumbwa katika uumbaji, halafu katika Mbingu mpya na nchi mpya utaondokewa usiwepo tena.

Nachosema k**a Muda/Wakati ukiondokewa kila kitu kinabaki palepale na kwa namna ile ile. K**a Bwana Mungu akiamua kuondoa Muda kwa mtu fulani duniani basi mtu huyo atabaki vile vile hata k**a ukija baada ya miaka mia mbili utamkuta vile vile! Ndivyo ilivyo, Malaika watakatifu waliumbwa maelfu ya miaka iliyopita, lakini kwa kuwa Bwana Mungu aliondoa Muda kwao wapo vilevile. Halikadhalika Watakatifu tutakaoingia Uzimani.
Kwa hiyo zile karatasi au lile lundo la nyasi k**a muda utaondolewa basi haijalishi moto utakuwa mkali kiasi gani, havitamalizika. Ndivyo itajavyokuwa Motoni!

Nilikuwa nakufikirisha tu. Sasa tuwapo hapa duniani yaani chini ya Mbingu, Muda ni kitu muhimu sana cha kuzingatia. Hatima yetu katika maisha yale yajayo yanategemeana ni jinsi gani tunavyotumia Muda wetu wakati huu.
Hivi unajua? Kuwa Ibilisi ni bingwa wa kuukomboa wakati?! Adui anatumia muda ule aliopewa kwa lengo moja tu, nalo ni kushindana na Mungu kwa kuwapotosha wanadamu. Kwa bahati mbaya wana wa Mungu wala hawana habari juu ya kuukomboa wakati.

Bado ninayo machache nadhani ya muhimu zaidi kukushirikisha katika Ujumbe huu, tukutane katika sehemu ijayo. Namuomba Mungu akueleweshe haya niliyoandika hapa, nimejitahidi kurahisisha lakini naona kwa wengine k**a bado ngumu kuelewa. Yafuatayo ni mepesi kueleweka. Ubarikiwe.

12/04/2021

JINSI YA KUUKOMBOA WAKATI - SEHEMU YA 3.

Ukichunguza vizuri Maandiko(Biblia),pia tukichunguza vizuri mfumo mzima wa maisha hapa ulimwenguni na vitu mbalimbali utagundua karibu kila kitu na kila jambo limepangiwa WAKATI WAKE wa kuwepo,kuishi,kutendeka, kutenda kazi nk. Katika vitu au bidhaa zinazotengenezwa na wanadamu, walichogundua wataalam au wanasayansi wetu ni juu ya Expired date yaani tarehe ya mwisho wa matumizi ya kitu au bidhaa. Lakini ukweli karibu kila kitu huku chini ya Mbingu, ukiacha Neno la Mungu ambalo ni la milele kina Expired date yake kwa namna mbalimbali.

Katika kitabu cha MHUBIRI 3:1 Biblia hapo inasema; "Kwa KILA JAMBO kuna majira yake, Na WAKATI kwa KILA KUSUDI chini ya Mbingu".
Halafu mstari wa 2 hadi wa 8 yanatajwa mambo machache kwamba yana WAKATI WAKE; "Wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa,... ".
Kisha mstari wa 11 ni wa kipekee sana, unasema; "KILA KITU (Mungu)amekifanya kizuri KWA WAKATI WAKE, TENA AMEIWEKA HIYO MILELE NDANI YA MIOYO YAO(Wamadamu),ila kwa jinsi mwanadamu asivyoweza KUIVUMBUA kazi ya Mungianayoifanya, tangu mwanzo hata mwisho".

Umeona Mandolin yanavyosema hapo juu? Kila kitu chini ya Mbingu yaani Duniani kimepangiwa Wakati wake, na kimefanywa kizuri kwa wakati wake. Kina muda maalum wa kuwepo kwake na kutenda kazi kwake. Halafu ule muda unaisha. Kila kitu na kila kiumbe kipo chini ya udhibiti wa Mungu Mwenyezi, Mbingu ndizo zinazotawala.
Hata Shetani/Ibilisi mwenyewe, pamoja na fujo zake zote, yupo chini ya udhibiti wa Mungu Mwenyezi, na tena amepangiwa muda maalum wa kufanya kazi zake, hatimaye muda huu utaisha na kutupwa kwenye mateso ya Moto wa milele. Shetani na mapepo yake yote wanalijua hilo. UFUNUO 12:12 Biblia inasema; "Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! Kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi AKIJUA YA KUWA ANA WAKATI MCHACHE TU:. Ibilisi anajua, mapepo pia wanajua kwamba wana muda kiasi fulani tu, na baadae nitakuonyesha sisi wanadamu pia tuna kiasi fulani cha muda tu katika mambo mbalimbali na maisha yetu kwa ujumla hapa duniani, na hivyo tunapaswa Kuukomboa Wakati maana ni mchache sana. Kuhusu mapepo tuangalie tena MATHAYO 8:28-29; "Naye(Yesu) alipofika ng'ambo katika nchi ya Wagerasi,watu wawili wenye pepo walikutana naye wanatoka makaburini, wakali mno, hata mtu asiweze kupita njia ile. Na tazama wakapiga kelele, wakisema,Tuna nini nawe Mwana wa Mungu? Je! Umekuja kututesa KABLA YA MUHULA(WAKATI) WETU?". Hili ni jeshi la mapepo ndani ya mtu. Sikiliza wanavyosema, kwamba kuna Muhula yaani Wakati wa wao kuteswa kutokana na uasi na uovu wao. Mashetani yote yanajua hayo na ndiyo maana yana hasira sana na chuki kuu dhidi ya Mungu na wanadamu. Na hii ndiyo hatima ya Shetani na Malaika zake;UFUNUO 20:10, "Na yule Ibilisi, mwenye kuwadanganya, akatupwa katika Ziwa liwakalo moto na Kiberiti,alimo yule Mnyama na yule Nabii wa uongo. Nao watateswa mchana na usiku hata milele na milele". Hiyo ndiyo hatima ya Ibilisi, mwenye kuwadanganya. Na ujue anapotajwa IbilIsi ni pamoja na Malaika zake yaani Mashetani yote(MATHAYO 25:41).

Kila jambo/kitu kina Wakati wake, isingekuwa rahisi kutaja jambo au kitu kimoja kimoja. Hata hivyo naomba tuliangalie hili kwanza ndipo tuendelee.
Katika kitabu cha YOHANA 4:35-36, Bwana Yesu anasema; "Hamsemi ninyi Bado miezi minne, ndipo yaja mavuno? Tazama, Mimi(Yesu) nawaambia, Inueni macho yenu myagazame mashamba ya kuwa yamekwishakuwa meupe, tayari kwa mavuno. Naye avunaye hupokea mshahara...".
Na hapa nataka niseme na Watendakazi wenzangu Shambani mwa Bwana. Anachosema Bwana wetu Yesu Kristo hapo ni kwamba, Tusiseme WAKATI wa mavuno bado, tusiseme mavuno ni mpaka miezi minne ijayo, bali mavuno yapo tayari na Wakati wake wa kuvunwa ndiyo SASA. Wakati mwingine tunadhani tuna muda mwingi kabisa wa kufanya kazi hii, lakini ukweli ni kwamba hatuna muda kabisa, Wakati umekwisha. Tujue kuna WAKATI uliopangwa kwa ajili ya Uvunaji, na Wakati huo ukipita hatutaweza tena kuvuna, na hao watu watakuwa wamepotea milele! Miezi kadhaa iliyopita nakumbuka maono niliyoyaona. Nilikuwa karibu na Shamba kubwa sana la ngano. Shamba lilikuwa kubwa sana katika eneo tambalale kiasi kwamba macho hayakuweza kuona mwisho wa Shamba au mashamba yale. Ngano yenye urefu wa k**a futi tatu na nusu, nzuri, safi, imekomaa vema, ikiwa tayari kwa kuvunwa ilikuwa imefunika Shamba lote hilo. Mimi nilikuwa pembeni au mwanzoni mwa Shamba hilo nikiwa nimeinama nafanya shughuri fulani hivi, hata sikumbuki shughuri gani?! Nilipoinua tena kichwa kungalia mashamba, nikashangaa kuona mashamba yale ya ngano yanaingia maji. Ni k**a ngano inanyeshewa na mvua nyepesi hivi. Mara ngano ile nzuri ikaanza kufubaa na kubadilika rangi na kuwa nyeusi nyeusi hivi. Mara ikaanza kurojoka ikiwa na mirenda mirenda! Ikawa imeharibika haifai tena!
Nachosema Watendakazi wa Bwana popote mlipo, kipaumbele chetu kwa sasa kiwe uvunaji. Mawazo yetu yanapaswa kufikiria ni jinsi gani tutaleta Ngano ghalani? Tutumie nguvu, rasilimali na chochote tulichonacho kuleta Mavuno gharani Kwani muda umekwisha. Huu si wakati wa kulumbana sisi kwa Sisi na kusak**ana. Kila mtu awe busy kukamilisha au kufunga hesabu yake, huku tukikumbuka kila mtu miongoni mwetu atatoa habari zake mwenyewe. Haina haja kufatiliana sana bali tufatilie nafsi zinazokeenda kupotea milele. Amen. ITAENDELEA. Ni Mimi ndugu yako Mchungaji Sume Mbena wa Huduma ya PENUEL, DSM.

Address

Tandale Kwa MTOGOLE
Dar Es Salaam

Website

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when UPAKO WA OMEGA posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Place Of Worship

Send a message to UPAKO WA OMEGA:

Share