17/04/2022
USIANGALIE UKUBWA WA UKUTA ULIOPO MBELE YAKO.
Usiuangalie ukubwa wa ukuta uliopo mbele yako, bali utazame ukuu wa Mungu, naye Mungu atakushindia.
Usiuangalie ukubwa wa mapito unayoyapitia, bali utazame ukuu wa Mungu, naye Mungu atakushindia.
Mungu ni mwenye uweza, hakuna jambo lililogumu mbele zake, yeye anaweza kila jambo. Inawezekana ukawa unapitia magumu mengi yanayokuzuia kufikia mafanikio, yanayokukosesha amani maishani mwako. Inawezekana ni maginjwa, matatizo ya ndoa, na mengine mengi. Wewe mtazame Mungu naye atakushindia.
Hehu tujifunze kwa wana wa Israeli, walipofika Yeriko, walizuiliwa na ukuta mkubwa kuingia ndani ya mji ili kuendelea na safari yao ya kuelekea Kanaani. Ukuta unakuzuia wewe ni hayo mapito unayoyapitia.
Usikate tamaa, Mungu anakuambia hivi k**a alivyosema na Yoshua, "BWANA akamwambia Yoshua, Tazama, nimeutia Yeriko katika mkono wako, na mfalme wake, na mashujaa wake." (Yoshua 6:2)
Kwahiyo nawe magumu hayo yamekwisha wekwa chini yako kuyamaliza, lililobaki ni wewe kufuata maelekezo ambayo Mungu anakupa ili kuyashinda hayo matatizo.
Wana wa Israeli walipewa jukumu la kuuzunguka mji ule kwa siku sita wakipiga tarumbeta na kelele mbele ya sanduku la agano. Na siku ya saba waliambiwa wauzunguke ule mji mara saba, makuhani saba wakipuliza tarumbeta wakiwa mbele ya sanduku la agano na wengine nyuma wakipiga kelele, na walipomaliza mizunguko yote ule ukuta ulianguka na wakauteketeza ule mji, waliopona ni familia ya Rahabu yule kahaba. (Yoshua 6)
Kwahiyo na wewe usilalamike, bali mwamini Mungu, mtii Mungu, mtegemee Mungu nawe utafanikiwa. Wala usione ugumu wa mambo ambayo Mungu atataka uyafanye ili kuyafikia mafanikio yako au ufumbuzi wa mapito yako.
Ndiyo maana Mungu aliwaambia wale watu wauzunguke mji, unafikiri Mungu asingeamua aungushe tu ule ukuta hata bila kuwaagiza kuuzunguka? Unafikiri angeshindwa? La! Hasha! Asingeshindwa. Bali alitaka aone imani yao kwake na utiifu wao kwake.
Unafukiri wale watu wangebaki kulalamika nje ya ukuta wangefanikisha kupita Yeriko, hapana, wasingeweza.
Ili uyashinde hayo mapito yako, ni lazima uchukue hatua.
(a) Mwamini Mungu kuwa anaweza hata yale yasiyowezekana (Yeremia 32:27, Luka 18:27)
(b) Ishi maisha matakatifu.(1Petro 3:13)
(c) Soma, jifunze, tafakari Neno la Mungu kila wakati, kwani huko ndiko kuna majibu ya mahitaji yako yote (Yoshua 1:8)
(c) Kila unalolifanya, lifanye kwa jina la Yesu, (Wakolosai 3:17)
(d) Omba bila kukoma,(1Wathesalonike 5:17)
Usimuogope adui yako, bali kabiliana naye kwa kumtegemea Mungu katika jina la Yesu Kristo aliye hai, maana yeye ni mshindi tangu enzi na enzi na hata milele, nawe utashinda.
Na ukisha shinda, watu wote watamtukuza Mungu aliye hai juu mbinguni na habari zake zitaenea kwa watu wote.
"Basi BWANA alikuwa pamoja na Yoshua; sifa zake zikaenea katika nchi ile yote." (Yoshua 6:27)
Kwahiyo mpendwa usiuangalie ukubwa wa ukuta(matatizo/mapito) uliopo mbele yako, bali utazame ukuu wa Mungu, naye Mungu atakushindia.
Mungu akubariki sana.